POLISI KISHAPU, WADAU WAADHIMISHA SIKU 16 ZA KUPINGA UKATILI WA KIJINSIA

Na  Malaki Philipo - Kishapu.

Dawati la Jinsia na Watoto Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia wameadhimisha siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia yakiongozwa na kauli mbiu 'Tupinge Ukatili wa Kijinsia, Mabadiliko yanaanza na mimi'.

Maadhimisho hayo yamefanyika leo Disemba 4,2020 kuanzia majira ya  saa mbili  asubuhi ambapo Jeshi la polisi kupitia Dawati la Jinsia na Watoto, wadau wa haki za binadamu na wanafunzi wa shule za msingi na sekondari, wamekutana na kufanya maandamano kutoka eneo la mto Tungu hadi shule ya sekondari ya Kishapu.

Wadau hao wamefanya maandamano ya amani kwa kupita katika mitaa mbalimbali ndani ya halmashauri ya wilaya hiyo wakiwa na mabango yenye jumbe  tofauti za kuhamasisha kupinga ukatili wilaya ya Kishapu.

 

Maandamano hayo ni nyenzo mojawapo katika  maadhimisho ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia, ambazo huadhimishwa  kila tarehe 25 ya  mwezi Novemba hadi tarehe 10 ya mwezi Desemba  kila mwaka, siku zenye lengo la kuendelea kuhamasishana kupinga vitendo vya unyanyasaji, ukandamizaji wa aina zote kati ya jinsi zote.

Mkuu wa Dawati la Jinsia na Watoto wilayani Kishapu Mkaguzi Msaidizi wa Jeshi la polisi Rose Mbwambo amesema maandamano hayo yanaakisi umakini wa dawati hilo katika kutoa elimu ya haki na uwajibikaji ili kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia na kwamba dawati hilo limekuwa likifanya kazi kwa weledi ambapo  kwa mwaka huu jumla ya wanaume tisa wamefungwa kifungo cha miaka 30 kila mmoja.

“Ukitazama takwimu za kuanzia mwezi Januari mwaka huu hadi mwezi Novemba tumepata taarifa 91 za ubakaji, na kati ya hizo taarifa watu 43 wamefikishwa mahakamani na tayari wanaume tisa wamefungwa miaka 30 kila mmoja, changamoto iliyopo ni ufichwaji wa mashahidi na kufanya mapatano ya kiamilia kumaliza kesi za namna hiyo lakini dawati linaendelea kuchukua hatua za kisheriia kwa wanaobainika na makosa hayo” amesema Rose.

Miongoni mwa wadau walioshiriki maandamano hayo ni shirika lisilo kuwa la kiserikali la REDESO, Benki ya NMB, Red Cross, TCRS, pamoja na watumishi wa halmashauri ya wilaya ya Kishapu, ambao kwa pamoja wamehimiza jamii kuacha ukatili kutokana na kusababisha madhara makubwa kiafya, kiuchumi, kimwili na hata kisaikolojia na kusema kwamba vitendo hivyo vimekuwa vikirudisha nyuma maendeleo hivyo basi jamii haina budi kuachana navyo.

Mkuu wa wilaya ya Kishapu Bi. Nyabaganga Talaba ambaye aliyapokea maandamano hayo amesema msimamo wa serikali ni kuhakikisha hali ya usawa, utulivu na amani katika kuvikabili vitendo vyote vinavyokiuka haki na utu wa mtu, na kuitaka jamii kuacha imani za kishirikina, imani zinazowaweka watoto  kwenye hatari ya kubakwa  na kundi la wazee katika hatari ya mauaji.

“Wilaya ya Kishapu si kwamba imeharibiwa na mila na desturi lakini uelewa wa baadhi ya wazazi kutambua mchango wa mtoto hasawa kike kwenye maendeleo lakini imani za kishirikina zimekuwa mwiba unaowatia hofu ya kubakwa kwa  watoto ama kulawitiwa lakini pia wazee kuingiwa na hofu ya kuuawa” amesema Talaba.

“Lakini serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo tutaendelea kutoa elimu ya kupinga ukatili na kuhakikisha tunachukua hatua kali za kisheria kwa wale wanaoendelea na vitendo hivyo kwa sababu zao, hatutawafumbia macho” ameongeza Talaba.

Maandamano ya dawati la jinsia na watoto wilaya ya Kishapu yametamatishwa na ugawaji wa taulo za kike, madaftari, kalamu pamoja na michezo mbalimbali ukiwemo mchezo wa mpira wa pete kati ya askari wa jeshi la polisi pamoja na wanafunzi wa shule ya sekondari ya Kishapu

.

Dawati la Jinsia na Watoto,wadau na wanafunzi wakiwa kwenye maandamano wakati wa maadhimisho ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia wilayani Kishapu

Maandamano yakiendelea.
Mkuu wa wilaya ya Kishapu, Nyabaganga Talaba (mwenye nguo nyeupe) akiwa kwenye maadhimisho ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia
Mkuu wa wilaya ya Kishapu, Nyabaganga Talaba akizungumza kwenye maadhimisho ya siku 16 za kupinga ukatili dhidi ya wanawake na watoto.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments