RAIS MAGUFULI AMTEUA TENA KASSIM MAJALIWA KUWA WAZIRI MKUU TANZANIA

Rais John Magufuli amemteua tena mbunge wa Ruangwa, Kassim Majaliwa kuwa Waziri Mkuu wa Tanzania.

Jina la Majaliwa limesomwa leo Alhamisi Novemba 12, 2020 bungeni mjini Dodoma na Spika Job Ndugai ili liidhinishwe na chombo hicho cha Dola.


Uteuzi huo unamfanya Majaliwa kuendelea na wadhifa aliokuwa nao kuanzia mwaka 2015 hadi Novemba 5, 2020 ulipokoma mara baada ya Rais Magufuli kuapishwa kuwa kiongozi mkuu wa nchi katika uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma.

Mara baada ya mpambe wa rais kuingia bungeni na bahasha yenye jina hilo na kumkabidhi Ndugai, alianza kuisoma na kutaja jina la Majaliwa na kusababisha wabunge kulipuka kwa shangwe.

Wabunge walinyanyuka kwenye viti vyao na kumfuata Majaliwa aliyekuwa ameketi kiti cha nyuma bungeni na kuanza kumpongeza huku wakiimba na kupiga makofi.


Spika Ndugai alimtaka Majaliwa ambaye alikuwa amekaa kiti cha nyuma, kwenda kuketi mbele kwenye nafasi yake. Majaliwa alifanya hivyo huku akiendelea kupongezwa na wabunge.



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments