KATIBU MKUU WIZARA YA MADINI PROF. MSANJILA AFUNGUA FURSA KWA KAMPUNI YA AGA BULLION KUWEKEZA KWENYE SEKTA YA MADINI NCHINI

Katibu  Mkuu wa Wizara ya Madini Prof. Simon Msanjila leo Novemba 12, 2020 amekutana na kufanya mazungumzo na kampuni ya AGA Bullion kutoka Nchini Uturuki  ofisini kwake Mtumba jijini Dodoma ambayo imeonesha nia ya kuwekeza kwenye sekta ya madini Nchini.


Katibu Mkuu Msanjila aeleza Tanzania ina masoko mengi makubwa ya Dhahabu  kuanzia mkoani Geita, Mwanza, Kahama na Chunya ambayo AGA Bullion wanaweza kuwekeza, kununua na kusambaza dhahabu kwa wingi hapa nchini.  Msanjila ametaka kampuni ya AGA Bullion kuwafikia wachimbaji wadogo na kati na kutoa mfano wa mgodi wa dhahabu wa Busolwa ambao unafanya kazi vizuri.


Amesisitiza Uwekezaji unaopangwa kufanyika na  kampuni ya AGA Bullion usilenge  kwenye ununuzi na usambazaji wa dhahabu pekee bali kuwekeza pia kwenye madini mengine yanayopatikana nchini yakiwemo  madini ya Tanzanite yanayopatikana mkoani Manyara, vilevile  kupata leseni ili waweze kuchimba  madini  nchini. 


Prof. Msanjila ameitaka Kampuni ya Aga Bullion kukutana na wadau mbalimbali wa sekta ya Madini  wakiwemo  Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) ambao hutoa huduma na ushauri wa kitaalam na kiufundi katika sekta ya madini wakiwemo wachimbaji wadogo kwenye nyanja za kijiolojia, Tume ya Madini na kukutana na Shirikisho la Vyama vya Wachimbaji Wadogo wa Madini (FEMATA),  ili waweze kujadili pamoja.


Kwa upande wake Mkurugenzi Mwanzilishi wa AGA Bullion, Sarp Tarhanaci amemueleza Katibu Mkuu Prof. Msanjila kuwa Kampuni ya Aga Billion inamiliki viwanda viwili vya usafirishaji wa dhahabu (Refineries) katika nchi za Umoja wa Falme za kiarabu (Dubai) na Uturuki, wanauzoefu katika ununuzi wa dhahabu kutoka katika mataifa mbalimbali kama vile Ghana, Burkina Faso, Peru, Malaysia na Uturuki.


Mkurugenzi Mwanzilishi Sarp Tarhananci akijibu hoja ya Katibu Mkuu kuhusu kukutana na wadau wengine wa Sekta ya Madini amesema tayari kampuni hiyo tarehe 10/11/2020 imekutana na kufanya mazungumzo na Tanzania Chambers of Mines (TCME) ambapo imepokea taarifa za uzalishaji na mauzo ya dhahabu, Tarehe 11/11/1010 ilikutana na Mkurugenzi wa Masoko ya Kifedha  wa Benki Kuu ya Tanzania ili kueleza nia yake ya kutaka kutoa huduma ya usafirishaji wa dhahabu, bima na kutafuta masoko ya kimataifa ya dhahabu iliyosafirishwa kwa gharama ya 0.5% hadi 0.8% ya thamani ya madini hayo.


Aidha amesema, kampuni ya AGA Bullion kwa kiasi kikubwa imemueleza Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini dhamira ya kufanya biashara ya madini ya dhahabu kutoka wa wachimbaji wadodo, pamoja na wachimabji wa kati ikiwemo kuwawezsha mitaji ya fedha ili waweze kuzalisha zaidi. Pia kampuni hiyo imezungumzia namna ya kuanzisha kiwanda cha  uongezaji thamani madini ya dhahabu (jewellery industry) kwa kutengeneza bidhaa zake kama vile pete, herein na mikufu.

Vilevile, kampuni hiyo imeeleza nia yake ya kutoa ushauri kwa Benki Kuu ya Tanzania, kuhusu namna ya kununua dhahabu kwa wachimbaji wadogo na kuwaweesha kifedha pamoja na utunzaji dhahabu kwenye accredited vaults za kimataifa kabla ya kuuza. Hata hivyo, Benki Kuu ya Tanzania ilieleza kampuni hiyo kuipatia taarifa zaidi za huduma zao.


Kikao hicho pia kimehudhuriwa na kamishina wa Madini Muhandisi David Mulabwa, Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu Issa Nchasi na wadau kutoka AGA Bullion kwa pamoja wamehaidi kuwekeza katika biashara ya madini hususan dhahabu  nchini.



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments