MARRY NYAGABONA MGOMBEA UBUNGE NCCR MAGEUZI TARIME MJINI ASEMA HAKUNA CHAMA CHENYE HATIMILIKI NA TARIME


Mgombea ubunge jimbo la Tarime mjini kupitia chama cha NCCR Mageuzi Marry Nyagabona akiwaomba kura wananchi wa mtaa wa Rebu Senta
Mgombea ubunge jimbo la Tarime mjini kupitia chama cha NCCR Mageuzi Marry Nyagabona akiwaomba kura wananchi wa mtaa wa Rebu Senta
Elias Nyagabona akimuombea kura mkewe Marry Nyagabona   Mgombea ubunge Tarime Mjini kupitia Chama cha NCCR- Mageuzi

Na Dinna Maningo, Tarime
Mgombea ubunge jimbo la Tarime mjini kupitia chama cha NCCR - Mageuzi Marry Nyagabona amesema kuwa hakuna chama chochote cha siasa chenye hatimiliki Tarime, kuwa ndicho kinafaa kuongoza ubunge kwani wananchi ndiyo wapiga kura wanaoamua kumchagua nani bila kujali chama.

Marry aliyasema hayo jana wakati wa kampeni zake mtaa wa Rebu Senta wakati akiwaomba wananchi kumchagua awe mbunge kupitia chama hicho.

Alisema kuwa baadhi ya wagombea wamekuwa na imani kubwa ya kushinda wakidhani kuwa kwa kuwa wapo kwenye vyama vikubwa hivyo ushindi ni lazima kwao.

"Tufanye kampeni salama hakuna chama chenye hatimiliki na Tarime, bali ni ya wananchi wao ndiyo wataamua wampigie mtu gani,kuna watu wanasema eti wasipotangazwa watatumia  nguvu,wengine wanasema usipochagua upinzani maendeleo hayaji si kweli na kwanini kampeni zisababishe tuchukiane" alisema Marry.

Alisema kuwa katika hospitali ya wilaya ya Tarime kumekuwa na changamoto ya uhaba wa dawa ikiwemo wodi ya wazazi na watoto nakwamba wakimchagua atahakikisha anaisemea kero hiyo bungeni pamoja na kero ya maji ndani ya mji wa Tarime .

"Chagueni mtu ambaye atawasaidia kuleta maendeleo mtu anasema asipotangazwa kitaeleweka wewe unajihakikishiaje kuwa wewe ndiyo utashinda!NCCR - Mageuzi ni chama cha Utu na utu ni binadamu,utu ni kumjali mwenzako na kumthamini" alisema.

Marry aliongeza kuwa kila mgombea anafaa kuwa mbunge hivyo ni vyema wananchi wakasikiliza sera za wagombea na siyo kuangalia chama atokacho.

"Viongozi wa dini tuiombee nchi yetu maana mamlaka inatoka kwa Mungu,mpeni Marry Nyagabona mama asiye na mkorogo,nimbaya sana kwenda kugombea ukiwa unajiamini kuwa utashinda unapogombea kuna mawili kushinda au kutishinda na ujiandae kisaikolojia kwa lolote litakalotokea" alisema Marry.

Mme wa mgombea huyo Elias Nyagabona akimuombea kura mkewe alisema kuwa ni vyema kutomchagua mtu wa kusababisha matatizo kati yake na Serikali iliyopo madarakani kwani hakuna Mbunge ambaye anaweza kuleta maendeleo jimboni kwake bila kushirikiana na Serekali iliyopo madarakani.

"Tuache ushabiki,tuache kupotoshwa hakuna mbunge wakufanya maendeleo bila kushirikiana na Serikali mkimchangua Marry Nyagabona atashirikiana na Serikali iliyopo madarakani ataongea na Waziri wa Afya,Waziri wa maji ili kuhakikisha kero zinatatuliwa" alisema Nyagabona.

Nyagabona aliwataka vijana wa Tarime kutotumika vibaya na wanasiasa kuivuruga amani ya Tarime na wafanye kampeni za amani zisizowagawa kwakuwa wote ni wana Tarime na Tarime ni ya watu wote.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments