KATAMBI ASHINDA UBUNGE SHINYANGA MJINI....CCM YANYAKUA KATA ZOTE ...SALOME MAKAMBA AKAMATWA

Patrobas Katambi

Na Damian Masyenene, Shinyanga
MGOMBEA Ubunge Jimbo la Shinyanga Mjini kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Patrobas Katambi ametangazwa mshindi wa ubunge baada ya kupata kura 31,831.

Katambi ametangazwa mshindi wa kinyang'anyiro hicho leo Oktoba 29, 2020 na Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo la Shinyanga Mjini, Geofrey Mwangulumbi, huku mpinzani wa karibu wa Katambi, Salome Makamba wa Chadema akiambulia nafasi ya pili kwa kupata kura 16,608.

Wagombea wengine katika kinyang'anyiro hicho walikuwa ni Godwin Makomba (ACT Wazalendo) aliyepata kura 883, Charles Shigino wa NCCR Mageuzi (133), Abdallah Issa Sube (Demokrasia Makini) kura 99, Yahya Khamis wa UDP kura 69 na Malengo Elias wa TLP kura 65.

Msimamizi huyo wa uchaguzi ameeleza kuwa katika zoezi la upigaji kura Jimbo la Shinyanga Mjini, wapiga kura walioandikishwa ni 120,944, idadi ya waliojitokeza kupiga kura ni 50,453, idadi ya kura halali ni 49,688 na zilizo haribika ni 765.

Katika hatua nyingine, Mwangulumbi amebainisha kuwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimeshinda viti vyote vya udiwani katika kata 17 za jimbo hilo.
Mgombea Ubunge Jimbo la Shinyanga Mjini kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Salome Makamba 

Wakati huo Jeshi Polisi mkoani Shinyanga linamshikilia Mgombea Ubunge wa Jimbo la Shi nyanga Mjini kwa tiketi ya CHADEMA, Salome Makamba kwa tuhuma za kumshambulia msimamizi wa uchaguzi kituo cha kupigia kura cha Bugweto B, Farida John na kumuumiza.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana usiku na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, ACP Debora Magiligimba  tukio hilo limetokea Oktoba 28, mwaka huu saa mbili usiku , ambapo Makamba aliomba aone matokeo na baada ya kutoridhika nayo aliyachana na kuanza kumshambulia msimamizi huyo wa uchaguzi akiwa na wafuasi wake.

ACP Magiligimba amesema baada ya kupata taarifa za tukio hilo, jeshi la polisi lilimsaka mtuhumiwa na kumkamata na upelelezi ukikamilika atafikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazomkabili.

CHANZO - SHINYANGA PRESS CLUB BLOG


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments