WAKULIMA WA PARACHICHI WAPATIWA ELIMU

WAKULIMA wa Parachichi katika mji wa Mafinga Wilayani Mufindi Mkoani Iringa  wamepatiwa elimu ya Kilimo bora cha zao hilo ambalo hivi sasa lina soko kubwa ndani na nje ya nchi.

Elimu hiyo imetolewa na Kampuni ya Agrigrow Tanzania LTD yenye makao makuu yake katika Mji wa Morogoro ambayo wana lengo kuleta mageuzi makubwa katika kilimo hapa nchini.

Akizungumza katika mafunzo hayo Mkurugenzi wa maendeleo ya Biashara Wilson Kashanga Mbwambo amasema kuwa lengo la kuendesha mafunzo hayo ni kuwapatia mbinu za kilimo hicho wakulima ili kuweza kuongeza uzalishaji ambao unakubalika katika soko la kimataifa

Hata  hivyo amewataka wakulima hao kuchagua mbegu bora hasa pale wanapotaka kuanzisha vitalu vya miche ya parachichi kwani hiyo ndiyo hatua muhimu ambayo itamfanya mkulima kupata faida kwa kile anachozalisha.

Katika hatua nyingine ameongeza kuwa hivi sasa kampuni hiyo itahakikisha wanatoa elimu mara kwa mara sambamba na kuwapatia virutubishi asilia katoka Agrigrow ambavyo vitawaongezea uzalishaji

Kwa upande wake Mkurugenzi mtendaji wa Mji wa Mafinga Saada Mwaruka amaesema kuwa katika kuunga Mkono uzalishaji wa parachichi hivi sasa wanaeeneo lenye ukubwa hekari 50 ambazo zitatumika kama shamba darasa kwa wakazi wa Mji  huo.

Nao baadhi ya wakulima wamesema kuwa hivi sasa wanakabiliwa na changamoto ya kupata miche bora ya zao hilo ambalo linawangezea kipato kikubwa kutokana na kuwa na soko la uhakika.

Hata hivyo wameomba elimu hiyo itolewe mara kwa mara pamoja na wataalam kufika katika mashamba ili kuangalia namna wanavyo hudumia mashamba yao ya parachichi

Akizungumzia suala la  Mbegu pamoja na miche bora ya parachichi Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Gerald Kusaya amesema kuwa hivi sasa  vituo vya utafiti wa Kilimo katika mikoa hiyo vimeshaanza kuuza miche ambayo ni bora na yenye kuongeza uzalishaji.

Mafunzo hayo ya Kilimo bora cha parachichi yaliyoandaliwa na Kampuni ya Agrigrow Tanzania LTD yenye makao makuu yake katika Mji wa Morogoro yaliweza kuwajengea uwezo wakulima katika kukabiliana na magonjwa na wadudu wasumbufu katika zao hilo pamoja na mbinu za kujikinga nao.

Hata hivyo wameahidi kuendelea kutoa elimu hiyo kwa wakulima wa Mikoa hiyo ya nyanda za juu kusini ili kuweza kuona faida ya kilimo cha parachichi ambacho kitaongeza kipato kwa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527