MAVUNDE, DITOPILE WAAHIDI DODOMA KUONGOZA KWA WINGI WA KURA ZA RAIS MAGUFULI OKTOBA 28

 Mgombea Ubunge Jimbo la Dodoma Mjini CCM, Anthony Mavunde (kushoto) akimnadi Mgombea Udiwani Kata ya Nkuhungu, Daud Mkhandi wakati wa uzinduzi wa kampeni za Udiwani kwenye Kata hiyo.
 Mgombea Ubunge Viti Maalum CCM kupitia Wanawake Mkoa wa Dodoma, Mariam Ditopile akihutubia kwenye uzinduzi wa kampeni za Udiwani Kata ya Nkuhungu ambapo alifika kumuombea kura Mgombea Urais wa CCM, Dk John Magufuli,  Mgombea Ubunge Jimbo la Dodoma, Anthony Mavunde na Mgombea Udiwani wa Kata hiyo, Daud Mkhandi.
Wafuasi wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Kata ya Nkuhungu wakiwa kwenye uzinduzi wa kampeni za Udiwani wa Kata hiyo ambapo mgombea wao Daud Mkhandi alikua anazindua kampeni zake.

Charles James, Michuzi TV

DODOMA lazima iongoze! Hayo ni maneno ya wagombea Ubunge Anthony Mavunde anayegombea Jimbo la Dodoma Mjini na Mariam Ditopile ambaye anagombea viti maalum wanawake mkoa wa Dodoma.

Wagombea hao wametamba kuwa ni lazima Jiji la Dodoma liongoze kwa kumpa kura nyingi za ndio mgombea Urais wa Chama cha Mapinduzi ©️ Dk John Magufuli katika uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba 28 mwaka huu.

Akizungumza katika uzinduzi wa kampeni za Udiwani Kata ya Nkuhungu, Mavunde amesema kwa maendeleo makubwa ambayo Jiji la Dodoma imeyapata kwa kipindi cha miaka mitano ya Magufuli wananchi wa Dodoma wana kila sababu ya kumpa kura nyingi Dk Magufuli.

Amesema ndani ya miaka mitano hii Rais Magufuli ameliheshimisha Jiji la Dodoma kwa kuhamishia shughuli zote za kiserikali jijini hapa jambo ambalo limechangia ukuaji wa kasi wa maendeleo.

" Dodoma ya sasa hivi inang'ara, miundombinu ya barabara imeenea na kutufanya Jiji letu kuongoza kwa mtandao wa lami kulinganisha na maeneo mengine nchini, Stendi ya Kisasa ametujengea ambayo inakua miongoni mwa stendi bora kabisa ukanda huu wa Afrika Mashariki.

Ndugu zangu nachowaomba ifikapo Oktoba 28 nendeni mkampe kura nyingi za ndio Dk Magufuli ili aimalizie kazi kubwa ambayo alishaianza ya kutuletea maendeleo na kututumikia sisi watanzania, " Amesema Mavunde.

Kwa upande wake Ditopile amewataka akina Mama kujitokeza kwa wingu siku ya kupiga kura ili wakamchague Magufuli kwa kura nyingi za kishindo kutokana na mambo makubwa aliyoyafanya kwa miaka mitano ya kwanza.

" Ndugu zangu wa Dodoma aliyotufanyia Magufuli ndani ya miaka mitano hii yangeweza kufanywa kwa miaka 20 lakini yeye katumia miaka mitano tu, leo Nchi haina mafisadi, umeme unawaka kila mahali, maji yamefika kila eneo na watoto wetu wanasoma bure.

Ni Dk Magufuli ambaye ametufanya Nchi yetu izidi kung'ara kwenye uchumi kwa kufikia uchumi wa kati lakini pia akipandisha kipato cha mwananchi mmoja mmoja hasa ikizingatia namna alivyopambana na janga la Corona na kulishinda bila kufungia watu ndani kama Nchi zingine," Amesema Ditopile.

Katika mkutano huo Mavunde aliwataka wananchi wa Kata ya Nkuhungu kumchagua Daud Mkhandi ili awe Diwani wao kwani ndie mgombea pekee mwenye sifa ya kuwatumikia wananchi.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments