SIMBA QUEENS NAYO YATWAA UBINGWA WA LIGI KUU YA WANAWAKE TANZANIA

Wachezaji wa Simba Queens wakishangilia ushindi

Timu ya Wanawake ya Simba Queens imefanikiwa kunyakua ubingwa wa Ligi Kuu ya Wanawake Tanzania Bara (Serengeti Lite Premier League)  baada ya kuichakaza bila huruma Baobab Queens kutoka Dodoma kwa mabao 5-0 katika mchezo uliopigwa Uwanja wa Uhuru leo Jumatano Agosti 5,2020.
 Hii ni mara ya kwanza kwa timu hiyo kutwaa ubingwa huo ikiondoa ufalme uliokuwa umewekwa na JKT Queens ambao walikuwa walitwaa ubingwa huo kwa miaka miwili mfululizo (2017/2018 na 2018/2019). 

Simba Queens ilikuwa inahitaji pointi tatu ili kufanikiwa kutwaa ubingwa huo ambapo kwa matokeo haya imefikisha pointi 53 ambazo haziwezi kufikiwa na timu nyingine. 

Katika mchezo wa leo, mabao ya Simba Queens yaliwekwa nyavuni na Nahodha Mwanahamisi Omari aliyefunga magoli mawili, Oppah Clement, Dotto Evarist na Mlinda mlango Zubeda Mgunda atupatia bao la tano kwa mkwaju wa penati dakika ya 55 kufuatia Mwanahamisi kufanyiwa madhambi ndani ya 18. 
Kikosi cha Simba Queens

Huu ni msimu wa tatu wa Simba Queens kwenye ligi kuu ya wanawake Tanzania bara, ambapo msimu wa mwaka jana ilimaliza katika nafasi ya tatu. Timu hiyo inamilikiwa na Klabu ya Simba, ambapo timu ya wanaume ya Simba SC imenyakua mataji matatu ambayo ni Ligi Kuu ya Vodacom, Ngao ya Jamii na Kombe la Shirikisho la Azam (ASFC).

Simba Queens itasafiri kesho Agosti 6, 2020 kuelekea jijini Mwanza kwa ajili ya mechi mbili zilizosalia za kumalizia msimu dhidi ya Alliance na TSC Queens.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527