MAKADA 99 WAJITOKEZAKUGOMBEA UBUNGE KATIKA MAJIMBO YA MSALALA,USHETU NA KAHAMA MJINI...VIJANA WATIA FORA



Naibu Waziri wa Ujenzi Eliasi John Kwandikwa (kulia) leo Julai 15 mwaka 2020 akirudisha fomu za kuomba ridhaa ya kuteuliwa kuwa Mbunge wa Jimbo la ushetu kwa katibu wa CCM wilaya ya Kahama Emanuel Mbamange. Picha zote na Salvatory Ntandu 
Meneja wa Benki ya CRDB kanda ya Magharibi Benjamini Ngayiwa akipokea fomu ya kugombea ubunge katika jimbo la kahama mjini kutoka kwa katibu wa CCM wilaya ya Kahama Emanuel Mbamange.
Mbunge wa Jimbo la Msalala Ezekiel Maige leo Julai 15 amechukua fomu za kuomba ridhaa ya kugombea Ubunge wa Jimbo la Msalala kulia ni katibu wa CCM wilaya ya Kahama Emanuel Mbamange.
Mtendaji wa Kata ya Chela John Mahona akipokea fomuza kuomba ridhaa ya kugombea ubunge wa jimbo la msalala kutoka kwa katibu wa CCM wilaya ya Kahama Emanuel Mbamange.

***

Na Salvatory Ntandu - Kahama
Jumla ya Wanachama 99 wa Chama cha Mapinduzi (CCM) wamejitokeza kugombea nafasi za Ubunge katika Majimbo ya Msalala,Ushetu na Kahama Mjini ikiwa ni siku ya pili tangu kuanza zoezi la utoaji fomu za kuwania nafasi Udiwani na Ubunge katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Mwezi Oktoba mwaka huu huku vijana wakionekana kuhamasika kwa wingi ikilinganishwa na uchaguzi uliopita.

Akizungumza na Waandishi wa Habari leo baada ya kukamilisha siku ya pili ya utoaji wa fomu za ubunge na Udiwani Katibu wa CCM wilaya ya Kahama Emmanuel Lameck Mbamange amesema zoezi hilo linaendelea vizuri na vijana ndiyo kundi pekee lililotia fora katika zoezi la hilo huku wanawake 9 nao wakijitokeza kuwania nafasi za ubunge katika majimbo hayo.

Amesema kuwa katika Jimbo la Kahama Mjini mpaka sasa wamejitokeza wagombea 53 kati yao wanawake ni sita ambapo nusu ya waliochukua fomu ni vijana ikilinganishwa na uchaguzi uliopita jambo ambalo linaonesha kukua kwa Demokrasia ndani ya CCM mpya inayowavutia vijana wengi kikipenda chama hicho.

“Katika Jimbo la Msalala mpaka sasa kunawagombea 33 ambapo mwanamke ni mmoja huku Jimbo la Ushetu likiwa na wagombea 13 huku mwanamke akiwa ni mmoja ,natarajia mapaka tarehe ya mwisho wagombea wengi watajitokeza kuomba nafasi mbalimbali za Ubungea na udiwani ili waweze kuwatumikia wananchi katika maeneo yao,”alisema Mbamange.

Mbamange alisema kuwa mpaka sasa Jumla ya wagombea 18 wamesharudisha fomu baada ya kumaliza kujiza na kusisitiza kuwa wagombea wote wanapaswa kuzisoma fomu hizo kwa makini ili kuepuka usumbufu usiokuwa walazima kwani wapo baadhi wanajaza bila kinyume na utaratibu unaotakiwa.

“Lengo letu sio kuwakosesha pindi mnapojaza fomu zenu hakikisheni mnajaza kwa ufasaha na hata kama ikitokea umekosea kujaza usianze kunung’unika njoo ufisini tutakupatia fomu zingine ili ujaze kwa ufasaha na hii ndio demokrasia inayotakiwa ndani ya CCM mpya,’alisema Mbamange.

Katika hatua nyingine Mbamange amewataka wagombea kutojihusisha na vitendo vya kampeni kabla ya muda jambo ambalo linaweza kusababisha wakakosa sifa na kuondolewa katika nafasi wanazoziomba na badala yake wazingatie maelekezo yaliyotolewa na chama katika utekelezaji wa zoezi hilo.

“Msianze kujipitisha pitisha kwa wananchi kwa kutoa rushwa mamlaka zinazosimamia sheria zipo macho muda wote ukishachukua fomu jaza rudisha na kisha subiria maelekezo ya chama ili uwe salama hatupendi kusikia mgombea Fulani kakamatwa kwa kuhushishwa na vitendo vya rushwa,”alisema Mbamange.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527