RAIS MAGUFULI: MKAPA ALIKATAA KUZIKWA DODOMA


Rais John Magufuli amesema rais mstaafu wa awamu ya tatu, Benjamin  Mkapa alipenda nyumbani kwao Masasi ndiyo maana alikataa kuzikwa katika eneo lililotengwa jijini Dodoma kwa ajili ya viongozi wa ngazi za juu za serikali.

Magufuli amesema hayo leo Jumatano, Julai 29, 2020, katika Kijiji cha Lupaso, Masasi mkoani Mwtara wakati wa maziko ya  Mkapa.

“Tulipangiwa kuzikiwa Dodoma.   Mzee Mkapa akaniuliza, ‘Mlipanga maziko yawe Dodoma?  Mimi msinizike Dodoma.’  Nikasema, ‘wewe unataka wakuzike wapi?’  Akasema Lupaso.  Nikamuuliza Mzee Kikwete akasema ‘mimi mnizike Msoga’.  Mimi nilisema nitazikwa Chato.”

“Niliogopa kumuuliza Mwinyi azikiwe wapi kwa sababu alikuwa na miaka zaidi ya 90, nikaona nikimuuliza halafu likatokea la kutokea nitaonekana mimi nimemletea uchuro, nikaona hilo eneo labda atazikiwa Mzee Malecela kwa sababu ni wa hukohuko Dodoma. Kwa sababu hakuna anayetaka kuzikwa Dodoma lile eneo nikaamua kuwapa wananchi na tayari walishaanza kujenga."-JPM


Akizungumzia mazishi ya Mzee Mkapa, Rais Magufuli amewashukuru viongozi wa dini, Serikali na Watanzania kwa kushiriki kikamilifu kuupumzisha mwili wa kiongozi huyo mstaafu katika makazi yake ya milele.

“Tumekuja hapa kwa kazi moja ya kumuaga Mzee wetu Benjamin Mkapa ambaye ametimiza kazi yake kwa miaka 82, nipende kwa mara nyingine kuwashukuru Watanzania wote mahali pote walipo, lakini kuwashukuru sana viongozi wetu wa dini zote,” amesema Rais Magufuli


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527