RAIS MAGUFULI AWASHUKURU WALIOMDHAMINI, ASEMA ANA DENI KUBWA

Na Richard Mwaikenda,Dodoma.

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi  (CCM), Dk. John Magufuli amewashukuru sana wote waliojitokeza kumdhamini kwa kujaza fomu za kuomba kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania 2020, kupitia chama hicho.

Shukrani hizo alizitoa mara baada ya kurejesha fomu Makao Makuu ya CCM, jijini Dodoma, ambapo kwa kitendo hicho cha kudhaminiwa na zaidi ya wanachama milioni moja wa Tanzania Bara na Visiwani, amesema kinamfanya awe na deni kubwa kwao.

Pia, Dk. Magufuli aliwapongeza Wenyeviti wa CCM wa mikoa yote 32 kwa kazi kubwa waliyoifanya ya kufanikisha udhamini huo mkubwa, licha ya kupata lawama nyingi kwa waliojitokeza kudhamini lakini walikosa fursa hiyo.

Aliwaomba wanachama waliokuwa na nia hiyo, wasivunjike moyo bali udhamini huo wauweke kwenye kura endapo mikutano husika ya chama itampitisha kuwa mgombea urais wa Tanzania kupita chama hicho, ili akapambane na wagombea wa vyama vingine.

Pia aliwaomba wanachama wa vyama vingine wampigie kura wakati wa kinyang’anyiro hicho, ili awatumikie Watanzania kutimiza malengo waliyojiwekea pamoja na kukamilisha miradi mbalimbali waliyoianza katika Serikali ya Awmu ya Tano inayoongozwa na yeye, ikiwemo ya Reli ya Kisasa ya Mwendo Kasi (SGR), Mradi mkubwa wa umeme wa Mwalimu Nyerere Rufiji na miradi mingine mingi.

Kabla ya kurejesha fomu, lilifanyika tukio la wenyeviti wa mikoa mbalimbali ya Tanzania Bara na Visiwani kukabidhi fomu za waliomdhamini kutoka katika mikoa hiyo. Pi wenyeviti wa Jumuiya za chama hicho; Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), Umoja wa Wazazi Tanzania na Umoja wa Vijana (UVCCM), walikabidhi fomu za waliomdhamini Dk. Magufuli.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527