BENARD MEMBE APOKELEWA RASMI ACT WAZALENDO....HIZI NI KAULI ZAKE BAADA YA KUPOKELEWA


Aliyewahi kuwa Waziri wa Mambo ya Nje nchini na Mbunge wa Mtama kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Bernard Membe, amejiunga rasmi na chama cha upinzani cha ACT-Wazalendo na kueleza sababu ya kujiunga na chama hicho cha upinzani nchini,  huku akipokelewa na mamia ya wananchama na viongozi wa chama hicho leo Alhamisi Julai 16, 2020, kwenye ukumbi wa Mlimani City, Dar es Salaam.



Miongoni mwa viongozi waliompokea Membe ni Maalim Seif Sharrif Hamad, Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe, Kiongozi wa ACT-Wazalendo na Ado Shaibu, Katibu Mkuu wa chama hicho.

Pia, makamu wenyeviti wa chama hicho, Juma Duni Haji (Zanzibar) na Doroth Semu wa Bara.

Waziri huyo wa zamani wa mambo ya nje, alifukuzwa uanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) tarehe 28 Februari 2020 na Kamati Kuu ya chama hicho, kisha uamuzi huo kubarikiwa na Mkutano wa Halmashauri Kuu ya CCM (NEC), tarehe 10 Julai 2020.

Membe alifukuzwa kwa tuhuma za ukiukwaji wa maadili ya CCM, pamoja na kuonywa mara kadhaa, pasina kubadilika.

Akizungumza ukumbini hapo, Membe amesema, ; “Kwa hiari yangu nimeamua kujiunga katika familia kubwa ya ACT Wazalendo inayotaka mabadiliko yenye lengo la kuwanufaisha Watanzania wengi hasa wakulima, wafanyabiashara, watumishi wa serikali, wafanyakazi mbalimbali na wote wanaoitakia kheri Tanzania yetu. Nataka kupigania mabadiliko ya kweli ya hii nchi kupitia ACT na azma yangu itatimia.

“Sijawahi kuona kijana asiye na tamaa kama Zitto Kabwe,  unaweza ukafika wakati wa uchaguzi akasema hagombei, huyu hana tamaa lakini hatma ya nchi hii iko mikononi mwake; huyu ndiye jasiri kiongozi, usipoteze ujasiri ulionao sisi tuko hapa kukusaidia.

“Maalim Seif amenilea tangu mwaka 1984 nyie hamumjui sijawahi kuona mwana– CCM aliyeyevumilia yasiyovumilika kama huyu, CCM na ujanja wetu wote huko nyuma hatukumshinda huyu mzee siasa hizi anazijua vizuri simjui mtu wa kumfanananisha naye." Amesema Benard Membe.


Huku akishangiliwa,Mwanasiasa huyo ametoa wito kwa kambi ya upinzani nchini, kuungana kwa pamoja ili  kupata ushindi.



“Naomba nitoe wito kwa kambi yote ya upinzani, ni lazima tuungane, uchaguzi ni wetu mimi naomba kabisa tuungane vyama vyote kama walivyofanya TLP na Cheyo kuwaunga mkono wenzetu, tuungane, umoja ni nguvu


”Mkoa wangu wa Lindi na Mtwara hivi sasa wanasubiri kuhamia ACT hivi ninavyozungumza nina wanachama wa CCM wanataka wajiunge, lakini jumla yake tuna kadi zaidi ya Elfu nane zitakazomiminika kwangu ili nizirudishe CCM” - Amesema Membe


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527