MTANDAO WA JINSIA TANZANIA 'TGNP' WAMLILIA RAIS MSTAAFU BENJAMINI MKAPA ..."ALIWEKA MISINGI YA USAWA WA KIJINSIA'


Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP Mtandao Lilian Liundi na Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu Hayati Benjamin William Mkapa (kushoto)


Na Kadama Malunde – Malunde 1 blog 
Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) umeungana na Watanzania wote Kuomboleza kifo cha Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu Hayati Benjamin William Mkapa ukieleza kuwa Taifa limepoteza mtu muhimu ambaye alikuwa mstari wa mbele kuweka misingi ya usawa wa kijinsia na kuendeleza usawa wa kijinsia nchini Tanzania. 

Akitoa salamu za Rambirambi, Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Lilian Liundi amesema Rais Mstaafu BenjaminWilliam Mkapa atakumbukwa sana na Wanamtandao wa Jinsia Tanzania na wanaharakati wa haki za wanawake na ukombozi wa wanawake kwa mambo mengi aliyoyafanya katika kipindi chake kwa kuweka misingi ya usawa wa kijinsia. 

Liundi ameeleza kuwa, katika kipindi cha utawala wake Mkapa Mkapa aliweka misingi ya kuendeleza uswa wa kijinsia katika nchi ya Tanzania na kisera, kisheria na kitaasisi na aliruhusu ushiriki wa makundi mbalimbali katika kufikia misingi ya usawa wa kijinsia. 

“Mwaka 2019 katika Tamasha la Jinsia tulimkumbuka, tulimsherehekea na tulimpa zawadi Mhe. Benjamin William Mkapa kwa kuweka misingi ya kisera ili kuendeleza usawa wa kijinsia Tanzania hasa katika kuweka vipaumbele vile vinne, kuweka misingi ya utekelezaji wa Azimio la Beijing”, anaeleza Liundi. 

Anafafanua kuwa, kwa masuala ya Azimio la Beijing na Mpango kazi wa Beijing ambapo pamoja na jitihada ambazo ziliwekwa na Marais wa Awamu zilizopita, lakini Mheshimiwa Mkapa kile alichokifanya cha ziada ni utashi wa kisiasa kuangalia kwamba wanawake ambao walikuwa wanakwenda kule wanaweza kushiriki vizuri. 

“Vile vie wakati wanawake wanarudi kutoka Beijing kitu pekee alichokifanya Mkapa ni mapokezi ya wale wanawake. Tukumbuke wale wanawake kuna wengine waliambiwa waishie huko Uwanja wa ndege na ajenda yao ya Beijing lakini yeye aliwapokea wanawake wa Tanzania wakiongozwa na Balozi Getrude Mongella ambaye alimpa ushirikiano mkubwa na hata ukiangalia hotuba ya Mhe. Benjamin Mkapa alivyokuwa anazungumzia pamoja na yale maeneo manne ya kipaumbele ambayo tulikubaliana kama nchi kwamba ndiyo tutayapa kipaumbele wakati huo wa utekelezaji wa kusema RUDISHA BEIJING NYUMBANI, amesema Liundi. 

“Maeneo hayo ni uchumi na kuondoa umaskini lakini pia kulikuwa na suala la wanawake kushiriki katika siasa na uongozi lakini pia masuala ya elimu, sheria na haki za mtoto wa kike. Mambo haya aliyapa kipaumbele zaidi na baada ya hapo tuliona jinsi gani mazingira wezeshi yalitengenezwa katika nchi yetu, kisera, kisheria na kitaasisi ambapo kipindi hicho hata sera ya jinsia ilitengenezwa na hata yale madawati katika kila Wizara yalianzishwa na mambo mengine mengi ambayo yalitengenezwa kutekeleza mpango kazi wa Beijing”, ameongeza Liundi. 

Kwa upande wa Azimio la Jinsia na Maendeleo ukanda wa SADC, Liundi anasema Mkapa alikuwa mstari wa mbele sana katika nchi za SADC,Tanzania ilikuwa mojawapo wa nchi zilizosaini azimio hilo kipindi cha utawala wa Mkapa ambapo alijaribu kuweka misingi ya Kisera na kitaratibu namna ya kutekeleza na kipindi hicho ndipo hata ileile asilimia 30 ilianza. 

“Hata michakato ya mifumo ya sera kuu za maendeleo ambazo zilikuwa zinaendelea katika nchi zilikuwa na ushiriki mpana wa wanawake hata tukiangalia dira ya taifa ya mwaka 2020/2025 unaiona kabisa ina misingi ya kijinsia lakini haikuja hivi hivi iliruhusu ushiriki mpana wa wanawake, ushiriki mpana wa asasi za kiraia ndiyo maana ikawa namna ile”, anaeleza Liundi. 

“Hata tukiangalia MKUKUTA ya kwanza, tunaona kabisa kulikuwa na ushiriki mpana, TGNP na asasi zingine zilishiriki na ndiyo maana hata ukiangalia kwenye MKUKUTA ya kwanza masuala ya kijinsia yaliingia sana kwenye mpango wa ufuatiliaji kulikuwa na masuala ya kijinsia”,anasema Liundi 

Anasema pia katika ngazi ya Afrika, Maputo Protocal ilikuwa pia ni kipindi chake aliridhia ule mkataba ili kuendeleza usawa wa kijinsia huku akieleza kuwa hata kama kuna mapungufu katika utekelezaji lakini kwa upande wa awamu yake misingi iliwekwa imara zaidi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527