RAIS MAGUFULI ATANGAZA SIKU SABA ZA MAOMBOLEZO KUFUATIA KIFO CHA RAIS MSTAAFU BENJAMIN MKAPA


Mhe. Benjamin William Mkapa
Rais Magufuli ametangaza siku saba za maombolezo ya Kitaifa kuanzia leo Ijumaa Julai 24,2020 kufuatia kifo cha Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu wa Tanzania Benjamin William Mkapa kilichotokea Hospitali jijini Dar es salaam ambapo katika kipindi chote cha maombolezo bendera zote zitapepea nusu mlingoti.



KUZALIWA

Benjamin William Mkapa alizaliwa Novemba 12, 1938 huko Ndanda Masasi Mkoani Mtwara na Amefariki Julai 24, 2020 jijini Dar es salaam.

ELIMU

Mwaka 1952, akiwa na umri wa miaka 15, alikwenda Seminari darasa la nane. 

Mwaka 1957, alichaguliwa kwenda St. Francis College Pugu ambayo ilikuwa ni shule kuu ya Wakatoliki Tanganyika.
Baadaye alijiunga na Chuo Kikuu cha Makerere nchini Uganda, ambapo mwaka 1962 alihitimu shahada yake ya kwanza kwenye Lugha ya Kiingereza.

Mwaka 1963 alijiunga na Chuo Kikuu cha Columbia ambapo alipata shahada ya uzamili kwenye Mambo ya Kimataifa.

UONGOZI
Alitumikia nyadhifa mbalimbali serikalini ikiwemo kuwa mmoja wa maafisa mkoani Dodoma.

Katika kuitumikia nchi, mwaka 1982 Mwalimu Nyerere alimtuma kuongoza mpango wa Tanzania na Canada ambao ulilenga kujenga mahusiano katika nyanja mbalimbali ikiwemo Elimu na Uchumi.

Pia alikuwa kiongozi wa mpango mwingine wa nchi katika kutengeneza mahusiano ya kimaendeleo na Marekani kati ya mwaka 1983 na 1984.

KUONGOZA WIZARA 
Katika uongozi wa Serikali ya kwanza ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Mkapa aliteuliwa kuwa Mbunge na Waziri wa Mambo ya Nje na akahudumu kutoka mwaka 1977 - 1980.

Baadaye Aliteuliwa kuwa Waziri wa Habari na Utamaduni kati ya mwaka 1980 – 1982.
Marehemu Mkapa aliteuliwa tena kuwa Waziri wa Mambo ya Nje kati ya mwaka 1984 - 1990.

URAIS

Mwaka 1995, Marehemu Rais Benjamin Mkapa aliteuliwa na Chama Cha Mapinduzi kugombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Uchaguzi huo ndio ulikuwa wa kwanza chini ya Mfumo wa Vyama vingi vya siasa na alishinda na kutangazwa kuwa Rais wa Awamu ya Tatu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Novemba 23, 1995 akaapishwa.

Alihudumu Ikulu kwa miaka 10 kutoka mwaka 1995 - 2005.

NAFASI NYINGINEZO

• April 1972 Mwalimu Nyerere alimteua kuwa Mhariri Mtendaji wa Daily News
• Muda mfupi baadaye Mwalimu alimteua kuwa Press Secretary wa Rais. 

• Mwaka huohuo, Mwalimu alimuagiza aanzishe Shirika la Habari Tanzania – SHIHATA na kuwa Mtendaji Mkuu wake.

• Mwaka 1976 akamteua kuwa Balozi huko Nigeria
• Mwaka 1982 Aliteuliwa kuwa Balozi wa Canada 
• Mwaka 1983 – 1984 Aliteuliwa kuwa Balozi nchini Marekani

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527