MKATABA MPYA WALIOSAINI YANGA,GSM NA LA LIGA


Uongozi wa Klabu ya Yanga wakishirikiana na wadhamini wao Kampuni ya GSM Mei 31 wameingia mkataba wa misimu minne wa makubaliano ya kimaendeleo ya timu hiyo na kampuni La Liga .


Makubaliano ya kuingia mkataba huo yalifikiwa juzi kwenye Hoteli ya Serena, jijini Dar ambayo yatahusisha maendeleo ya mchezo wa soka nchini kupitia La Liga ambayo yanahusisha masuala ya ufundi na vifaa mbalimbali.

Klabu ya soka ya Yanga, mbali ya kufaidika na mfumo mpya wa uendeshaji, pia itapata fursa ya mafunzo kwa wachezaji, makocha na viongozi kutoka klabu ya Sevilla ya Hispania.


Mkataba huo ambao msingi wake ni kuifanya Yanga kuwa na mfumo wa kisasa wa uendeshaji, umeenda mbali zaidi ambapo licha ya kucheza mechi mbili kwa mwaka baina ya Sevilla na Yanga, pia utatoa fursa kwa wachezaji chipukizi kujiunga na shule ya michezo ya timu hiyo yenye historia kubwa ya soka.

Kwa mujibu wa ofisa habari wa Yanga, Hassan Bumbuli kutakuwa na mechi mbili kwa mwaka baina ya timu yao na Sevilla ambayo moja itafanyika Hispania na nyingine hapa nchini.

Malipo ya kwanza ya mkataba huo yanatarajiwa kufanyika kati ya kipindi walichoingia mkataba huo hadi Agosti 31, mwaka huu kwa Yanga na GSM kuilipa La Liga kiasi cha euro elfu 80 ambayo ni sawa na Sh milioni 204 baada ya makato iwapo yatatokea.

Wakati malipo ya pili ambayo yatafanyika msimu ujao katika kipindi kati ya Septemba mwaka 2020 hadi Juni 2021


Mbali ya mapendekezo ya mfumo wa uendeshaji, pia kutakuwa na suala mabadiliko ya Katiba ya klabu ambapo mpango wa klabu ya Yanga ni kuwahsirikisha wanachama na wadau wote kwa muda wa siku 21.

Mwenyekiti wa Yanga, Dk Mshindo Msolla alisema wawakilishi wa matawi kutoka kila pande za Tanzania watapata mafunzo maalumu jijini Dar es Salaam na kupewa makabrasha ambayo watayatumia kuendesha elimu ya mabadiliko hayo pindi watakaporejea kwenye matawi yao




Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527