CHADEMA YATANGAZA RATIBA KWA WAGOMBEA WA URAIS, UBUNGE NA UDIWANI KUPITIA CHAMA HICHO


CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimefungua zoezi la uchukuaji fomu za kugombea Urais wa Tanzania, ubunge na udiwani, katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020.


Ratiba hiyo imetolewa leo Jumatatu tarehe 29 Juni 2020 na Reginald Munisi, Mkurugenzi wa Uchaguzi Chadema, wakati anazungumza na waandishi wa habari, makao makuu ya chama hicho, Kinondoni jijini Dar es Salaam.

Munisi amesema, zoezi la uchukuaji na urejeshaji fomu ya urais wa Tanzania, litafanyika kuanzia tarehe 4 hadi 19 Julai 2020.

Amesema katika mchakato wa kumpata mgombea Urais wa Tanzania ndani ya Chama, mtia nia au wakala wake Julai 4,mwaka huu Chama hicho kitafungua mlango wa mtia nia au wakala wake kuchukua fomu za kugombea urais wa Tanzania kupitia Chama hicho.

Amesema fomu hizo za urais zitatolewa Makao Makuu ya Ofisi ya Chama hicho na kila mgombea atatakiwa kudhaminiwa na wanachama wasiopungua 100 kwa kila Kanda.

“Tunakanda 10 za CHADEMA Tanzania, nane zipo Bara na visiwani zipo kanda mbili, hivyo wagombea watapita na kuomba wadhamini katika kanda hizo na wadhamini hao hawapaswi kuwa ni wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Chama Taifa,”alisema na kuongeza kuwa;

“Mgombea wa nafasi hiyo au wakala wake atatakiwa kuwasilisha fomu za kuomba uteuzi Julai 19 mwaka huu na kuambatanisha viambatanisho vyote vilivyotajwa katika fomu na stakabadhi ya malipo ya fomu kwa Katibu Mkuu wa Chama,”amesema Munisi.

Aidha amesema Jula 22, mwaka huu Katibu Mkuu wa Chama hicho atawasilisha taarifa kuhusu mchakato huo kwa kamati kuu ya chama ambapo Kamati hiyo itapendekeza jina au majina ya wagombea kwenda Baraza Kuu na Mkutano Mkuu kwa ajili ya mapendekezo ya uteuzi wa mwisho .

Akizungumzia upande wa nafasi ya ubunge, amesema wagombea wa ubunge watatakiwa kujaza fomu za kuomba uteuzi wa kugombea nafasi hiyo ndani ya Chama.

Alisema fomu zao zitatolewa Julai 4, mwaka huu hadi Julai 10 kwa Tanzania Bara na Visiwani ambapo zitapatikana katika mtandao wa chama na Ofisi za Majimbo ya Chama hicho.

“Kamati Kuu ya Chama itafanya uteuzi wa wagombea wa nafasi ya ubunge Julai 30 hadi 31 mwaka huu,ambapo wagombea wataitwa na kuhojiwa juu ya uanachama wao na sera zao,”alisema na kuongeza

“Hatua ya pili majina yatakayoteuliwa yatapelekwa katika kura ya maoni kwa Mkutano Mkuu wa Majimbo kisha kurudishwa katika kamati tendaji ya Kanda na kufanya mapendekezo ya nani anafaa,”Amesema

Akizungumzia nafasi za Udiwani Munisi amesema utafiti wa kuwapata wagombea wa udiwani (Tanzania bara)utaendeshwa kwa kuzingatia sheria ya Chama huku kila mgombea akiitwa mbele ya kamati ya Utendaji kueleza taarifa zake.

Amesema fomu zao zitaanza kutolewa Julai 11, mwaka huu katika Ofisi za kata za Chama na kurudisha fomu Julai 17,mwaka huu nao watapigiwa kura ya maoni na Kamati ya Utendaji ya Jimbo ambayo itakaa na kufanya uthibitisho wa wagombea udiwani .


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527