WAZIRI KABUDI ASEMA ZAMBIA HAIJAFUNGA MPAKA WAKE NA TANZANIA....."HAWAJAFUNGA MPAKA NA NINA BARUA YAO WAMETUANDIKIA"


Serikali imewatoa hofu Watanzania na kusema kwamba Zambia haijafunga mpaka wake na Tanzania. Imesisitiza kuwa uhusiano kati ya nchi hizo ni mzuri.


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Profesa Palamagamba Kabudi, ametoa ufafanuzi huo jana Bungeni jijini Dodoma, wakati akihitimisha hoja za Wabunge waliojadili Bajeti ya Wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2020/2021.


" Nataka niwaambie Zambia haijafunga mpaka na Tanzania, narudia tena Zambia haijafunga mpaka na Tanzania ,haya si maneno yangu,ninayo barua kutoka kwa Waziri wa Mambo ya Nje nchini Zambia Joseph Malanji ambaye Mungu amemjaalia kujua lugha nyingi.

"Kwa hapa Tanzania anazungumza kinyakyusa , Kinyiha, Kinyamwanga, na jana na leo tumezungumza kwa Kiswahili. Naomba nisome barua yake japo ni jambo ambalo si la kawaida , ameniandikia barua ambayo imefika leo baada ya kufanyika kwa mazungumzo,"alisema Profesa Kabudi na kisha kuisoma barua hiyo iliyoandikwa kwa lugha ya Kingereza. 


Profesa Kabudi alifafanua kwa mujibu wa barua hiyo ambayo imefafanua kwa kina kuwa Zambia haijafunga mpaka, imeeleza kuwa Kamati ya timu ya watalaamu kutoka Tanzania na Zambia watakutana kwa pamoja kuweka mambo sawa na kisha huduma kurejea kama kawaida.

Aidha, Waziri Kabudi, amesema, kamwe Tanzania haitaruhusu maadui kutaka kuivuruga Jumuiya ya Afrika Mashariki.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527