VIFO VYA CORONA MAREKANI VYAFIKA 85,197


Vituo vya kuzuia na kudhibiti magonjwa nchini Marekani (CDC) vimetangaza vifo vipya 1,426 vinavyohusiana na Corona, na kufikisha jumla ya watu 85,197 waliofariki dunia tangu kuzuka kwa janga hilo.

Vituo vya CDC pia vimeripoti visa vipya 21,647 vya maambukizi ya virusi vinavyosababisha ugonjwa hatari wa Covid-19, na kufikisha jumla ya idadi ya visa 1,430,348 vya maambukizi nchini humo.

Wakati huo huo Shirika la Afya Duniani limeyataka mataifa kuchukua tahadhari za hali ya juu.

Katika mkutano na waandishi wa habari kwa njia ya video kutoka Geneva, Mkurugenzi wa dharura wa WHO, Dkt Mike Ryan ameonya dhidi ya kujaribu kubashiri ni lini virusi vya Corona vitatoweka.

"Ni muhimu kufahamu hili: Virusi vinaweza kuwa janga jingine katika jamii zetu, na virusi hivi huenda visiishe, " Dkt Mike Ryan amesema.

Hayo yanajiri wakati Ulaya imeanza kuchukua hatua za awali kuelekea kufungua mipaka yake ya ndani, baada ya miezi miwili ya vizuizi vya kukabiliana na janga la Covid-19, huku WHO ikiyataka mataifa kuchukua tahadhari za hali ya juu.



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527