TRUMP ATISHIA KUIONDOA MAREKANI KWENYE SHIRIKA LA AFYA DUNIANI WHO NA KUSITISHA MISAADA YOTE

Rais Donald Trump wa Marekani ametishia kuiondoa Marekani kwenye Shirika la Afya Duniani WHO, akidai kuwa taasisi hiyo ya kimataifa ni kikaragosi cha China.


Trump ametoa vitisho hivyo katika barua aliyomuandikia Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Afya Dunia, Tedros Adhanom Gabrayesus ambapo amesema, "Marekani itaikatia misaada WHO kikamilifu iwapo haitapiga hatua kubwa za kujiboresha ndani ya siku 30 zijazo."

Rais huyo wa Marekani ametuma ujumbe uliouambatanisha na nakala ya barua hiyo kwenye ukurasa wake wa Twitter na kuandika: Tunaipa WHO dola milioni 450 kila mwaka, lakini hawatutendei wema, wamekuwa wakitupa ushauri mbaya.


Hii ni katika hali ambayo, mwezi uliopita wa Aprili, Trump alitoa tuhuma kali  dhidi ya shirika hilo akidai kwamba linaipendelea China, na hivyo akachukua uamuzi wa kulitakia misaada ya kifedha.

Mbali na kuilaumu WHO, Trump pia amekuwa akidai kwamba China haikuweza kutoa kwa wakati muafaka taarifa za kuenea virusi vya corona wala kukabidhi takwimu sahihi za virusi hivyo kwa Shirika la Afya Duniani; ambapo pia alitishia kuwa huenda akaamua kukata uhusiano wa Washington na Beijing.

Hadi sasa Marekani ina visa 1,550,539 , vifo 91,985 na idadi ya wagonjwa waliopona ni 356,383


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527