MKUCHIKA AZINDUA BODI YA USHAURI YA WAKALA YA NDEGE ZA SERIKALI

 James K. Mwanamyoto – Chamwino Dodoma

Serikali imezindua Bodi ya Ushauri ya Wakala ya Ndege za Serikali ambayo itakuwa na jukumu la kumshauri Waziri mwenye dhamana juu ya namna bora ya kuboresha wakala hiyo ili kuwa na mipango na mikakati endelevu itakayoleta tija katika usafiri wa anga.

Akizindua bodi hiyo jana Ikulu ya Chamwino, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Kapt. (Mst) Mhe. George H. Mkuchika (Mb) ameitaka bodi kuhakikisha Tanzania inakuwa na Shirika la Ndege imara litakaloweza kushindana na mashirika mengine ya kikanda na kimataifa kwa kuanzisha na kuendesha safari nyingi za ndani ya nchi, za kikanda na za kimataifa.

Mhe. Mkuchika amesema, suala la kuimarisha usafiri wa anga kwa kulifufua Shirika la Ndege la Tanzania ni moja ya utekelezaji wa ahadi za Chama cha Mapinduzi iliyopo kwenye ilani yake ya Uchaguzi ya Mwaka 2015. Mhe. Mkuchika ameitaka Wakala ya Ndege za Serikali (TGFA) na Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) kufanya kazi kwa ushirikiano wenye tija ikiwa ni pamoja na kujengeana uwezo na uzoefu kiutendaji.

Aidha, Mhe. Mkuchika amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kulipa uzito mkubwa jukumu la usimamizi wa TGFA kwa kumteua Katibu Mkuu Kiongozi, Mhe. Balozi
Mhandisi John W. H. Kijazi kuwa Mwenyekiti ya Bodi ya Ushauri wa Wakala ya Ndege za Serikali.

Kwa upande wake, Mhe. Balozi Mhandisi John W. H. Kijazi, amemshukuru Mhe. Rais kwa kumuamini na kumpa jukumu la kuongoza bodi hiyo ili iweze kutekeleza majukumu yake kikamilifu.

Mhe. Balozi Kijazi ameahidi kutekeleza maelekezo yote yaliyotolewa na Waziri Mkuchika ili kuiwezesha Wakala ya Ndege za Serikali kutekeleza majukumu yake ikiwa ni pamoja na kuliimarisha Shirika la Ndege ya Tanzania kuwa imara na la kiushidani.

Wakala ya Ndege za Serikali ilianzishwa rasmi tarehe 17 Mei, 2002 kupitia Sheria ya Wakala za Serikali Na. 30 ya Mwaka 1997 kama ilivyorekebishwa Mwaka 2009. Wakala hii, ilikuwa chini ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ambapo tarehe 23 Aprili, 2018, Serikali iliamuia kuihamishia Ofisi ya Rais, Ikulu kwa Tangazo la Serikali Na. 252 la tarehe 8 Juni, 2018.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527