Mashambulizi makali ya waasi yaharibu Uwanja wa Ndege wa Tripoli Libya

Mashambulizi makali ya maroketi yaliyofanywa jana Jumamosi na waasi dhidi ya Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mitiga, jijini Tripoli, Libya yameua raia sita na kusababisha hasara kubwa kwenye uwanja huo.

Raia wengine kadhaa wamejeruhiwa katika shambulio hilo la waasi wanaoongozwa na Jenerali Khalifa Haftar ambao wanaungwa mkono na Saudi Arabia, Umoja wa Falme za Kiarabu (Imarati), Misri na baadhi ya nchi za Magharibi.

Waziri wa Mambo ya Ndani wa Serikali ya Mwafaka wa Kitaifa ya Libya inayotambuliwa kimataifa amesema kuwa, takriban maroketi 80 yamevurumishwa kwenye uwanja huo wa ndege, na kuteketeza ndege mbili aina ya Airbus, kusababisha moto katika maghala ya mafuta na kuteketeza magari ya Zima Moto.

Kwa upande wake, Waziri wa Uchukuzi wa Libya amesema, moja na ndege zilizoshambuliwa ilikuwa inajiandaa kupaa kuelekea Uhispania kwa ajili ya kuwachukua raia wa Libya waliokwama katika nchi hiyo ya Ulaya kutokana na janga la corona.

Uwanja wa Ndege wa Mitiga ndio pekee unaofanya kazi katika mji mkuu wa Libya, Tripoli. Hata hivyo, safari za abiria wa kawaida zilisimama tangu mwezi Machi kutokana na kushambuliwa mara kwa mara uwanja huo hata kabla ya nchi hiyo kuchukua hatua za kufunga maeneo ya nchi hiyo kutokana na corona.

-Parstoday


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments