KATIBU MKUU WIZARA YA KILIMO: SERIKALI HAITOONGEZA MUDA KWA WAKANDARASI WALIOZEMBEA KUMALIZA SKIMU ZA UMWAGILIAJI


Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Gerald Kusaya, leo (tarehe 19 Mei, 2020) ameonya wakandarasi wanne waliochelewesha kumaliza miradi ya ujenzi wa skimu za umwagiliaji zilizopo mkoa wa Morogoro.

Awali akifungua kikao hicho cha dharura alichokiitisha leo ofisini kwake Dodoma ili kuwapa nafasi Wakandarasi hao waseme kwa nini Wizara isivunje mikataba nao; Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo alieleza kusikitishwa kwa namna walivyoshindwa  kumaliza kazi ya ujenzi wa skimu za umwagiliaji  katika maeneo tofauti ya mkoa wa Morogoro ndani ya muda wa mikataba.

Wakandarasi walioitwa kujieleza Jijini Dodoma ni Kampuni ya Nakuro JV Comfix Engineering Ltd; Inayojenga Skimu ya umwagiliaji ya Njage (Kilombero); Comfix Engineering inayojenga skimu ya umwagiliaji ya Msolwa Ujamaa (Kilombero) Kampuni nyingine ni Gopa Construction (T) Ltd inayojenga skimu ya umwagiliaji ya Kigugu (Mvomelo) na ya mwisho ni Kampuni ya Lukulo Company Ltd; Inayojenga skimu ya umwagiliaji ya Kilangali (Kilosa).

“ Sisi serikali tunataka miradi yote ikamilike kwa haraka na ubora.Hatuwezi kuongeza miezi sita ya nyongeza kwa kazi hii iliyochukua muda mrefu kukamilika” alisema Kusaya

Baada ya majadiliano yaliyochukua masaa kadhaa Wakandarasi wote waliomba kuongezewa muda kwa vipindi tofauti ili wamalizie miradi hiyo ambayo ipo kwenye hatua tofauti; ombi ambalo lilikataliwa na Katibu Mkuu Kusaya.

Katibu Mkuu ameongeza kuwa suala la kuongezewa muda lina mchakato wake na kwamba Wakandarasi wote  walitakiwa kumaliza kazi zao kwa wakati na kukabidhi Miradi yote terehe 30 Aprili, 2020 na kuongeza kuwa kuongeza muda ni kukiuka masharti ya mikataba walijoingia na Mteja wao (Serikali).

Aidha Katibu Mkuu huyo Alitoa onyo kwa mkandarasi wa skimu ya Njage iliyopo Kilombero kuacha mara moja kutumia saruji iliganda kwani haina ubora

“ Natoa onyo kwa kampuni ya Nakuro JV Comfix kuacha mara moja kutumia sariji iliyoganda kujeng skimu yetu pale Njage.Nitachukua hatua kali za kisheria ikiwa ni pamoja na kuvunja skimu hiyo endapo itaonekana haijakidhi ubora unaotakiwa.” Alisisitiza Katibu Mkuu Kilimo

Mwisho


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527