WAZIRI WA AFYA UMMY MWALIMU AWATAKA VIONGOZI WA DINI WAEPUSHE MISONGAMANO KWENYE NYUMBA ZA IBADA ILI KUKABILIANA NA CORONA


Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu ametoa rai kwa viongozi wa dini nchini kuhakikisha wanaepuka misongamano kwenye nyumba za ibada hasa katika kipindi hiki cha kuelekea sikukuu ili kujikinga na maambukizi ya virusi vya corona.


Waziri Ummy amewaomba viongozi hao kuhakikisha waumini wenye dalili za kikohozi, mafua na homa wanabaki nyumbani.

Ameyasema hayo wakati akizungumza na waandishi wahabari jijini Dar es Salaam leo Alhamisi Aprili 9, wakati wa kikao cha kitaifa cha viongozi wa dini kilichozungumzia jinsi ya kujikinga na maambukizi ya virusi vya corona.

Amesema hadi sasa kuna idadi ya wagonjwa 25 na taarifa nyingine ataitoa mchana baada ya kupata maelezo watalaamu waliopo maabara.


"Ugonjwa tumeletewa kutoka nje, hivi sasa takwimu za jana, juzi na wiki iliyopita tumeanza kuambukizana wenyewe kwa wenyewe. viongozi wangu wa dini naomba niliweke wazi its no longer imported cases, tumeanza local transmission.



"Ndani ya siku chache tutaingia katika community transmission. Maana yake tutapata mgonjwa ambaye hajui ugonjwa ameupata wapi? Sasa hivi amekuja mtu anamuambikiza fulani ndio maana tunafanya contact (muingiliano) kujua.

Amefafanua kuwa hatua ya maambukizi katika jamii ni ngumu aliyeambukizwa amepewa na nani na kwamba ndani ya siku chache inawezekana tukaingia katika hatua hiyo.



"Lazima niwaambia ukweli nisiwafiche soon (karibuni), tutaingia kwenye community transmission. Bado tunatakiwa kuchukua tahadhari na kuongeza juhudi za kukabiliana na ugonjwa huu," amesema Ummy.

Waziri huyo amesema ni wajibu wa kila kiongozi wa dini kuhakikisha wanaendesha ibada katika utaratibu na mazingira yasiyo hatarishi ili kujikinga dhidi ya virusi vya corona, akisema makongamano ya dini sio muhimu kwa wakati huu.



“Ni mategemeo yetu viongozi wa dini kuepuka mikusanyiko ya watu wengi, tunategemea kupata ushirikiano wenu kuhakikisha kuwa ibada zinaendeshwa katika mazingira ambayo si hatarishi, rais ameeleza kuwa serikali haitafunga nyumba za ibada lakini ni wajibu wetu kuangalia sasa tutafanya ibada kwa namna ambayo si hatarishi kwetu na kwa waumini.

“Kingine tunachoomba ni kuwepo utaratibu wa kupunguza waumini wakati wa kutoka na kuingia katika nyumba za ibada, kuwa na ibada fupifupi zinazofanyika mara kwa mara, kufanya usafi wa mara kwa mara kwenye nyumba za ibada na utakasishaji,” amesema.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527