UMMY MWALIMU: TUMEANZA KUPATA MAAMBUKIZI YA NDANI YA VIRUSI VYA CORONA, TUONGEZE TAHADHARI

Na Mwandishi Wetu WAMJW Dar es Salaam
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu amesema Tanzania imeanza kupata maambukizi ya Virusi vya Corona ya ndani kuanzia maambukizi yaliyopatika tarehe 08/04/2020.


Amesema kuwa tahadhari kubwa inahitajika katika kuhakikisha kuzuia kuendelea kwa maambukizi ya kijamii itasababisha kuongezekana kwa kasi ya maambukizi katika jamii.

Ameyazungumza hayo leo jijini Dar es Salaam wakati wa mkutano na viongozi wakuu wa madhehebu ya dini katika kujadiliana namna ya kukabiliana na maambukizi ya virusi ya Corona nchini.

Ameongeza kuwa Serikali itatangaza hivi karibuni wananchi kuchukua tahadhari kwani tafiti zinaonesha virusi vya Corona vinaweza kusambaa na kuambukizwa kwa njia ya hewa hivyo maelekezo ya kutumia barakoa yatatolewa ili kuondokana na maambukizi.

“Tafiti zimeonesha kuna uwezekano wa Virusi vya Corona vinaweza kuenezwa kwa njia ya hewa hivyo tutaleta muongozo wa kuanza kutumia Barakoa (Mask) kwa jamii ili kuzuia  maambukizi kuenena kwa njia ya hewa” alisema

Aidha amewataka viongozi wa dini kutoa rai kwa wazazi na walezi kuwalinda watoto kutowaruhusu Watoto kuzurula na kuhangaika ovyo mitaani ili kupunguza uwezekano wa kuongezeka kwa maambukizi ya virusi vya Corona.

“Imani ya watanzania wengi kufikiri kuwa hatuwezi kupata maambukizi ni suala sahihi tunaweza kupata maambukizi kama watu wengine wanavyopata” alisema.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Maendeleo ya Jamii Dkt. John Jingu amesema kuwa viongozi ni watu muhimu katika kuleta mabadiliko katika Jamii yetu kwani wanasikilizwa zaidi na waumini katika sehemu za ibada.

Ameongeza kuwa lengo ni kuwashirisha viongozi wa kidini katika kuhakikisha wanatimiza wajibu wao katika kuhakikisha maambukizi ya virusi vya Corona yanatokomea nchini.

"Viongozi wa kidini ni watu muhimu sana katika mapambano katika kuondokana na maambukizi ya Virusi vya Corona nchini tunaomba mtusaidie katika hili" alisema

Naye Mkurugenzi wa Shirika la World Vision Gilbert Kamanga amewaomba vingozi wa dini kutofanya suala la virusi vya Corona kuwa la kisiasa bali waunganishe nguvu pamoja ili kuondokana na maambukizi ya virusi vya Corona.

Ameongeza kuwa jamii inatakiwa kupewa elimu kila mahali ikiwemo katika nyumba za ibada ambapo watu wengi ukusanyika pamoja kuabudu itakuwa sehemu sahihi kufikisha ujumbe kuhusu kuondokana na maambukizi ya virusi vya Corona.

"Viongozi wetu wa dini nawaomba tushikamane katika hili kwani virusi vya Corona ni hatari sana lakini tukisimama pamoja hakika tutafanikiwa katika kutokomeza virusi vya Corona" alisema

Akitoa salam za mkoa wa Dar es Salaam Mganga Mkuu wa Mkoa huo Dkt. Rashid Mfaume amesema mkoa umejidhatiti katika kupambana kwa kuenea na maambukizi ya Virusi vya Corona mkoani humo kwa kuzingatia maelekezo yanayotokea na wataalam wa Afya  na Serikali kwa ujumla.

Naye Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Alhaji Musa Salum amesema janga la Corona ni kubwa na kama watu wa imani tunaamini katika kumuonba Mwenyezi Mungu na tunaamini litatokomea.

Pia amemshukuru Rais John Magufuli kuendelea kuruhusu ibada kuendelea katika kama kawaida ni jambo ambalo litasaidia kuzidisha maombi katika kupambana na Virusi vya Corona.

Mkutano huu kati ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu na viongozi wakuu wa madhehebu ya dini umekuja wakati Tanzania ikiendelea kupambana na maambukizi ya virusi vya Corona huku ikiwa na jumla ya watu 25 waliombukizwa virusi hivyo.

MWISHO.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527