MWANAMKE AMUUA MME WAKE BAADA YA KUMALIZA KUFANYA NAYE MAPENZI MME WA PILI AKIWA NJE


Na Kadama Malunde – Malunde 1 blog 

Mwanamke aitwaye Nyamizi Madereke (41) mkazi Kitongoji cha Kitangili kata ya Kitangili katika Manispaa ya Shinyanga amemuua mmewe Paul Isack (45) kwa kumchoma kisu kifuani muda mfupi baada ya kumaliza kufanya naye tendo la ndoa huku mme wa pili akiwa nje ya nyumba.


Inaelezwa kuwa tukio hilo limetokea Aprili 2, 2020 majira ya saa tatu usiku nyumbani kwa Paul muda mfupi baada Paul kumnyang’anya Nyamizi kitenge chake alichokuwa amevaa na kubakiza skin tight pekee kutokana na ugomvi uliotokea kati ya Paul na mme mwenzake aitwaye Kulwa mkazi wa Matanda baada ya Nyamizi kumaliza kufanya mapenzi na Paul. 

“Paul na Nyamizi wote ni wakazi wa Kitongoji cha Kitangili ambao wameoana miaka mingi iliyopita lakini mara nyingi wamekuwa wakiachana na kurudiana na hivi karibuni walivyoachana,Nyamizi aliamua kupanga kwenye nyumba nyingine akaanza kuishi na mwanaume mwingine aitwaye Kulwa katika nyumba hiyo aliyopanga” ,amesimulia Mwenyekiti wa serikali ya Mtaa wa Kitangili, Habiba Jumanne alipozungumza na Malunde 1 blog 

“Siku ya tukio Paul alitoka nyumbani kwake majira ya saa 11 jioni na kwenda nyumbani kwa Nyamizi ambako alikuwa akiishi na Mume wake wa sasa Kulwa. Alipofika nyumbani kwa Nyamizi,Kulwa alikuwa bado hajarudi kutoka kazini ndipo Paul aliingia ndani na kumkuta Nyamizi alimsalimia na baada kusalimia aliomba apatiwe tendo la ndoa ombi ambalo lilikubaliwa na Nyamizi wakaanza kufanya humo ndani”,ameeleza Mwenyekiti wa mtaa. 

“Baada ya Paul na Nyamizi kumaliza kushiriki tendo la ndoa walitoka ndani na kumkuta Kulwa yupo nje ya nyumba,Paul alimshika Nyamizi mkono na kumuamuru waondoke kitendo kilimkera Kulwa naye akaamua kumshika mkono wa pili akimtaka Nyamizi arudi ndani”,anaeleza Jumanne 

Amesema kutokana na hali hiyo Paul na Kulwa walianza kupigana baada ya kuchoshana wote kwa pamoja Paul, Kulwa na Nyamizi waliambatana kwenda nyumbani kwa Paul lakini wakati wakiendelea na safari,ghafla Paul alimnyang’anya Nyamizi kitenge alichokuwa amejifunika na kukimbia nacho. 

“Nyamizi aliamua kwenda nyumbani kwa Paul ili kufuata kitenge chake alichodai kilikuwa kimefungwa shilingi 5,000 na alipofika akamkuta mdogo wake na Paul aitwaye Mathias Isack na mama yao hata hivyo ambao walimuuliza kuwa anamtafuta nani kwani walishamkataza kufika hapo nyumbani ndiyo Nyamizi alijibu anamtafuta Paul. 

“Baada ya muda mfupi Paul alirejea nyumbani kwake akiwa hana kitenge na alipomkuta Nyamizi walianza kupigana mbele ya mdogo wake na mama yake na wakiwa wameangushana ghafla Paul alisikika akilalamika Umenichoma Kisu umeniumiza’,ameeleza. 

Kufuatia tukio hilo walifanya jitihada za kutafuta pikipiki ili kumpeleka hospitali kupata matibabu lakini Paul alifariki dunia akiwa njiani. 

Mwenyekiti huyo amesema kutokana na tukio hilo walimkamata Nyamizi na kumpeleka katika kituo cha polisi. 

Jumanne amesema mazishi ya Paul Isack yamefanyika siku ya Jumapili,Aprili 5,2020.


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP Debora Magiligimba Paulo Isack alifariki dunia katika hospitali ya rufaa mkoa wa Shinyanga akiwa anapatiwa matibabu baada ya kuchomwa kisu kifuani na na mwanamke huyo ambaye ni mpenzi wake eneo la kitangili majira ya saa 1:30 usiku.

“Chanzo cha tukio ni wivu wa mapenzi kwani marehemu alikwenda nyumbani kwa mtuhumiwa ambaye walishaachana naye takribani wiki mbili zilizopita akilazimisha warudiane na alale nyumbani hapo huku akimtuhumu kuwa amepata mwanaume mwingine”,amesema Kamanda Magiligimba.

Amesema mwili wa marehemu umehifadhiwa katika hospitali ya rufaa mkoa wa Shinyanga kwa ajili ya uchunguzi na kwamba mtuhumiwa  amekamatwa.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527