MMILIKI WA MABASI YA J4 JIJINI MWANZA AHUKUMIWA ADHABU YA KUNYONGWA HADI KUFA


Mahakama Kuu imemhukumu kunyongwa hadi kufa mmiliki wa kampuni ya mabasi ya J4 Express, Jumanne Mahende (45) baada ya kumtia hatiani kwa kuwaua kwa kuwapiga risasi watu wawili.

Hukumu hiyo ilitolewa jana na Jaji Sam Rumanyika baada ya kukubaliana na upande wa mashataka kwamba umethibitisha kosa bila kuacha shaka.

Kwa mujibu wa mashtaka, mshtakiwa aliwaua kwa risasi wafanyakazi wake wawili; Ally Abeid na Claudia Kalwanda wakiwa eneo la ofisi zake Nyakato Goma jijini Mwanza Julai 13, 2015.

Jaji Rumanyika alisema kwa kuzingatia ushahidi wa watu 12 na vielelezo tisa vya upande wa mashtaka na ushahidi wa mtu mmoja wa upande wa utetezi, mahakama imejiridhisha kwamba mshtakiwa alitenda kosa hilo kwa makusudi.

Upande wa utetezi ulikuwa na shahidi mmoja ambaye alikuwa mshtakiwa mwenyewe, katika utetezi wake aliieleza mahakama kwamba aliua bila kukusudia. Hata hivyo, Jaji Rumanyika aliukataa utetezi huo kulingana na nguvu iliyotumika kuua.

“Kuna misingi minne hapa ambayo najielekeza nayo, kwanza kuangalia silaha iliyotumika, kama mshtakiwa alionyesha kujutia baada ya tukio; kuchukua tahadhari kabla ya kutenda jambo hili; lakini haya yote hakuyafanya kwa hiyo hakuna shaka namtia hatiani kwa maujia ya kukusudia.
Advertisement

Hapa adhabu yake ni kifo kwa kila kosa (makosa mawili) lakini zote zinaenda kwa pamoja, kwa hiyo utanyongwa hadi kufa,” alisema Jaji Rumanyika.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527