KAMATI YA HESABU ZA SERIKALI ZA MITAA YAKOSHWA NA MIRADI YA MAENDELEO MAKAMBAKO


Na Amiri Kilagalila,Njombe 
Kamati ya kudumu ya bunge ya hesabu za serikali za mitaa LAAC imeridhishwa na hali ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya halmashauri ya mji wa Makambako mkoani Njombe,na kuahidi kuongeza nguvu serikalini ili kusaidia ukamilishwaji wa ujenzi wa majengo ya makao makuu ya halmashauri hiyo.

Makamu mwenyekiti wa kamati ya LAAC Abdalah Chikota ambaye ni mbunge wa jimbo la Nanyamba amesema hali ya utekelezaji wa miradi katika halmashauri ya mji wa Makambako inaridhisha lakini mradi wa ujenzi wa makao makuu umechelewa kukamilika kutokana na changamoto ya upatikanaji wa fedha pamoja na kuto tekelezwa majukumu ya kimkataba na mkandarasi aliyeanza kushika mradi huo.

"Kamati imeridhishwa na hali ya utekelezaji wa miradi Makambako,lakini kuna mradi mmoja tumeona una changamoto ule wa ujenzi wa makao makuu,lakini changamoto hizi zimesababishwa kwanza na upatikanaji wa fedha ule wa mradi ni wa mda mrefu na haujakamilika na fedha zilikuwa zimetolewa kidogo ukilinganisha na ghalama za mradi,lakini changamoto nyingine ni ya mkandarasi hakutekeleza majukumu ya kimkataba hivyo halmashauri ikalazimika kuvunja mkataba na sahizi wameamua kujenga kwa force akaunti"alisema Abdalah Chikota

Vile vile Chikota amesema kamati imedhamilia kuishauri serikali kupeleka fedha za kutosha katika halmashauri ya mji wa Makambako ili mradi uweze kukamilika ma kuepusha matumizi ya ofisi hizo zilizoanza kutumika ilihali majengo hayajakamilika.

Awali baadhi ya wajumbe wa kamati ya LAAC akiwemo Zainab Bakari na Ezekiel Maige mbunge wa Msalala,kutokana na taarifa ya mkurugenzi wa halmashauri hiyo Paul Malala walihoji sababu za kuchelewa kwa mradi huo ambapo  mhandisi wa halmashauri ya mji wa Makambako Emilly Maganga akifafanua kuwa miongoni mwa sababu ni pamoja na ucheleweshwaji wa fedha ,kuezekwa kwa paa bila utaratibu pamoja na kufanyiwa usanifu upya wa mradi.

"Usimamizi wa mradi huu wakati tunaanza ulisimamiwa na mwandisi kutoka mkoa wa Njombe na kutoka halmashauri ya mji wa Makambako lakini wakati wa utekelezaji wa awamu ya pili tulimwajili mshauri wa mradi ambaye ni Biko na alipokuja akabaini kuna baadhi ya maeneo anatakiwa kuyaimarisha kwa hiyo alifanya usanifu upya na katika usanifu alioufanya mojawapo ikawa ni kuongeza nguzo katika baadhi ya maeneo"alisema Emilly Maganga

Hata hivyo mkurugenzi wa halmashauri ya mji wa Makambako Paulo Malala amesema licha ya kuwa jengo hilo limeanza kutumika ikiwa bado halijakamilika,fedha zinazohitajika kwa sasa ili kukamilisha ujenzi ni kiasi cha shilingi bilioni moja na milioni mia tatu.

Kamati ya kudumu ya bunge ya hesabu za serikali za mitaa LAAC imefanikiwa kupitia na kukagua jumla ya miradi mitano ya ujenzi wa ofisi za halmashauri ya mji wa Makambako,ujenzi wa hospitali ya  halmashauri unaoendelea katika kata ya Mlowa,Ujenzi wa kituo cha afya Lyamkena kinachoghalimu milioni 400,Majengo mawili ya madarasa ya shule ya sekondari Lyamkena pamoja choo yaliyojengwa na TASAF pamoja na mradi wa maji wa Kiumba na kuridhishwa na miradi hiyo.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527