WIZARA YA KILIMO YASEMA TANZANIA HAIJAVAMIWA NA NZIGE WA JANGWANI

Waziri wa Kilimo Mhe.Japhet N.Hasunga (Mb) jana Jumapili anawafahamisha wakulima na wananchi kwa ujumla kuwa taarifa zinazoenea kwenye baadhi ya vyombo vya habari na mitandao ya kijamii kuhusu uwepo wa nzige wa Jangwani nchini  hususan mkoa wa Kilimanjaro siyo za kweli.


Mhe.Hasunga amesema hayo wakati alipoongea na kituo cha Televisheni ya Taifa (TBC1) na kusema “ hakuna taarifa za kitaalam zilizothibitisha uwepo wa nzige kwenye mikoa ya Kilimanjaro na Arusha. Ila ni kweli Kuna nzige wameonekana Kaunti ya Kajiado nchini Kenya takribani kilomita 50 toka mpakani na Tanzania”  alisema Waziri wa Kilimo

Wataalam wa Wizara ya Kilimo kwa kushirikiana na Shirika la Chakula na Kilimo duniani (FAO) linaendelea na ufuatiliaji wa viashiria vya uwepo wa nzige na tayari hatua za awali za kuwadhibiti endapo wataingia nchini zimechukuliwa. Hatua hizo ni pamoja na Mashirika ya kimataifa ambayo sisi ni wanachama kutuahidi ndege tatu maalum za kunyunyizia dawa na uwepo wa dawa za tahadhali kwenye mikoa ya Arusha, Manyara na Kilimanjaro.

Wizara inatoa wito kwa wakulima, maafisa ugani na kilimo na wadau wote wa kilimo kuendelea kutoa ushirikiano wa taarifa sahihi kwa serikali endapo kutajitokeza viashiria vya nzige kwenye maeneo ya mashamba.

Aidha,vyombo vya habari vinasisitizwa kutoa taarifa sahihi na za ukweli ili kuepusha sintofahamu kwa wakulima.

Imetolewa na ;
Prof. Siza D. Tumbo
KAIMU KATIBU MKUU


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post