CHAMA CHA WAFANYABIASHARA WANAWAKE TANZANIA 'TWCC' CHATOA MAFUNZO KWA WAJASIRIAMALI KAGERA


Kaimu Mkurugenzi Mtendaji Chama Cha wafanyabiashara wanawake Tanzania (TWCC ) Mwajuma Hamza wakati akitoa mafunzo kwa wajasiariamali wanawake Manispaa ya Bukoba mkoani Kagera.
Na Ashura Jumapili, Bukoba
Chama cha Wafanyabiashara Wanawake Tanzania (TWCC) kimetoa mafunzo kwa Wajasiriamali Wanawake mkoani Kagera kuhusu namna ya kutumia fursa za kibiashara maeneo ya mipakani sanjari na kujua sheria,kanuni na taratibu za kuvuka mipaka ambapo jumla ya wanawake 100 watakaonufaika na mafunzo hayo ya siku nne.

Kaimu Mkurugezi Mtedaji wa Chama hicho Mwajuma Hamza,alisema lengo la chama hicho ni kuwaunganisha Wanawake wote Wajasiriamali wa Tanzania ili wawe na umoja ,nguvu ,sauti na mikakati ya pamoja katika biashara hivyo wanawafundisha wanawake namna ya kufanya biashara za mipakani ,kutumia fursa za biashara za Jumuia ya Afrika Mashariki,kanuni,taratibu na sharia za kufanya biashara maeneo ya mipaka.

Alisema soko la Afrika Mashariki ni kubwa na Tanzania inazalisha vitu vingi ambavyo nchi jirani hawazalishi hivyo hiyo pia ni fursa moja wapo kwa wajasiramali hao.

“Tunataka Wanawake waingie kwenye uchumi wa viwanda na waweze kuzalisha Zaidi bidhaa zenye tija na ubora unaokubalika na soko la kimataifa”,alisema Hamza.

Alisema chama hicho kilianza mwaka 2005 kimesajiliwa kwa mujibu wa sharia na kina Zaidi ya wanachama ( 5000 )nchi nzima pia kina ofisi mikoa 10 na mwezi Machi mwaka huu wanatarajia kufungua ofisi nyingine Mkoani Kagera.

 Alisema pia wanawasaidia wajasiriamali wanawake kupata taarifa za masoko ,kuzalisha bidhaa zenye ubora zinazokidhi soko la ndani n nje ya nchi, kuongeza uzalishaji na jinsi ya kuweza kupata mitaji ya kuendesha biashara zao.

Alisema wamezindua mfumo wa kuripoti vikwazo vya kibiashara maeneo mbalimbali ikiwemo maeneo ya mipaka.

Mgeni rasmi katika mafunzo hayo,Afisa biashara mkoa wa Kagera ,akimuawakilisha katibu tawala mkoani humo Prof.Faustine Kamuzora, alisema Tanzania ina fursa nyingi zinazotokea duniani ambapo inapakana na nchi nane.

Tendega,alisema mkoa wa Kagera unapakana na nchi nne ,Jumuia ya Afrika Mashariki ina watu wasiopungua milioni 190 ni ukanda wa watu wengi na kudai kuwa Watu hao ni soko kwa bidhaa zinazozalishwa Tanzania.

Alisema Kanda ya ziwa inachukua asilimia 14 ya watu wote wa nchi hii pia ni fursa ya kuweza kupeleka bidhaa huko.

Alisema hali ya hewa ya mkoa wa Kagera ni nzuri ina misimu miwili ya mvua na pia kuna ziwa Victoria linafaa kwa shughuli mbalimbali za kilimo na uvuvi.

Alisema mkoa unakabiliwa na changamoto moja ya uzalishaji mdogo wenye viwango hafifu .

Alisema ili kukabiliana na uzalishaji mdogo ni vyema wajasiriamali wakaungana na kushirikiana kuongeza tija katika uzalishaji wa bidhaa mbalimbali.

“Chuki kwenye biashara ni mwiko,mshirikiane kuunganisha mawazo,nguvu na mitaji ili kuwa na mshikamano katika biashara zenye ubora na tija”,alisema Tendega.

Alisema Mkoa umefanya jitihada mbalimbali za kumkomboa mwanamke ikiwemo kuanzisha madawati mbalimbali ya mkoa na wilaya lengo likiwa kuwawezesha wanawake kiuchumi na kuwaweka pamoja kuchangamkia fursa mbalimbali.

Kaimu meneja wa shirika la kuhudumia viwanda vidogo vidogo (SIDO )Mkoani Kagera Peter Kilima,alisema wajasiriamali hao watapata fursa ya kujifunza na kuelewa pamoja na kukabiliana na changamoto za kibiashara wanazokutana nazo.

Kilima,alisema SIDO wamejipanga kuwasidia wajasiriamali katika kuwapatia mitaji kwa kutwapatia mikopo ya kiasi cha shilingi laki 5 hadi milioni moja.

Akiongea kwa niaba ya Wajasiriamali wenzake Jovita Banyeza ,alisema mafunzo hayo yatawasidia kutambua na kuibua fursa za kibiashara zilizopo mipakani.

Banyenza,alisema ndio mwanzo wa kuzifungua na kuwajibika katika fursa hizo za kibiashara kwa wanawake .

Alisema mikopo isiyokuwa na riba kwa wanawake inayotolewa na halmashauri imekuwa chachu kwa wafanyabiashara wanawake ambao sasa wameamka na kujikita katika biashra mbalimbali.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527