WAKULIMA WA MAHINDI TABORA WAOMBA KUPATIWA MBOLEA YA UREA

Na Salvatory Ntandu
Uhaba wa mbolea aina ya  UREA katika msimu wa kilimo wa mwaka 2019/20 mkoani Tabora  umetajwa kuchangia  wakulima wa zao la mahindi kuzalisha kwa kiwango cha chini na kusababisha baadhi ya wakulima kuiomba kampuni ya usambazaji pembejeo za kilimo ya PETROBENA kuanza kuwakopesha kwa msimu ujao.

Hayo yalibainishwa febuari sita mwaka huu na Wakulima wa zao hilo kwenye mkutano wa mkuu wa 27 wa chama kikuu cha wakulima wa Tumbaku kanda ya Magharibi (WETCU) ambapo walidai mwaka huu uzalishaji wa mahindi umeshuka kutoka na kukosekana kwa mbolea aina ya UREA.

Juma Madoshi ni mmoja wa wakulima wa zao la mahindi mkoani humo alisema kuwa familia nyingi huenda zikakabiliwa na uhaba wa chakula mwaka huu kutokana na  uhaba wa mbolea hiyo na kuiomba kampuni ya usambazaji Pembejeo za kilimo ya PETROBENA kuwakopesha UREA kwa msimu ujao.

“Sisi wakulima wa zao la mahindi mwaka huu tutapata chakula kidogo,tumezoea kuzalisha kwa wingi,tunaiomba serikali kupita viongozi wetu wa chama chetu (WETCU) kufanya mazungumzo na PETROBENA ili msimu ujao tusipate changamoto hii” alisema Madoshi.

Nae Monika Manwali mkulima wa zao la tumbaku mkoani humo alisema awali walikuwa wanakopeshwa mbelea na kampuni za ununuzi wa zao hilo ambazo walikuwa wanazitumia katika kilimo cha cha mahindi lakini mwaka huu imekuwa tofauti ikilinganishwa mwaka huu ambapo utaratibu umebadilika.

“Tunaomba kukopeshwa mifuko miwili ya UREA ambayo inatosha kuitumia kwenye hekari mbili na itasaidia wakulima kupata mahindi  yakutosha ambayo yatasaidia familia zetu kuwa na uhakika wa chakula cha kutosha kwa mwaka mzima”alisema Manwali.

Akizungumza kwenye mkutano wa mkuu wa 27 wa chama kikuu cha wakulima wa Tumbaku kanda ya Magharibi (WETCU) mkuu wa mkoa wa Tabora Agrey Mwanri alizitaka kampuni za usambazaji wa pembejeo za kilimo kuhakikisha wanasambaza mbolea kwa wakati ili kwenda sambamba na msimu wa kilimo wa mwaka huu.

“Msimu wa kilimo umeanza muda mrefu sisi kama serikali hatukubali kuona wakulima wetu wanaendelea kuteseka kwa kukosa mbolea aina ya UREA licha ya kuwa na mashamba ya kutosha na nguvu kazi ipo”alisema Mwanri.

Katika hatua nyingine Mwanri alisema kuwa kwa msimu ujao wakulima watakaobainika mwaka huu hawajapanda miti katika mashamba yao hawataruhusiwa kulima zao la tumbaku hivyo ni budi wakulima wote wakazingatia maelekezo ya serikali.

Mwisho.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post