TAIFA STARS YATUPWA KUNDI D FAINALI ZA CHAN 2020


Droo ya michuano ya Mataifa ya Afrika kwa wachezaji wa ndani CHAN 2020 imepangwa usiku wa jana, Februari 17, 2020 mjini Yaounde nchini Cameroon.

Katika droo hiyo, imeshuhudiwa timu 16 zikipangwa katika makundi manne yenye timu nne, ambapo Cameroon ambao ni wenyeji wa michuano hiyo, wakipangwa katika kundi A pamoja na timu za Mali, Burkina Faso na Zimbabwe.

Kundi B likiwa na timu za Libya, DR Congo, Congo Brazzaville, Niger na kundi C likihusisha timu za Morocco, Rwanda, Uganda, Togo.

Taifa Stars ambayo inayoshiriki michuano hiyo kwa mara nyingine ya pili tangu ilipofanya hivyo mwaka 2009 nchini Ivory Coast, imepangwa kundi D pamoja na timu za Zambia, Guinea na Namibia.

Kundi la awamu hii la Taifa Stars linaonekana kuwa ni jepesi kulinganisha na kundi ambalo alipangwa katika CHAN 2009, akipangwa na timu za Senegal, Zambia na wenyeji Ivory Coast. 

Taifa Stars iliondolewa katika hatua ya makundi baada ya kushinda mechi moja dhidi ya Ivory Coast na kufungwa mechi moja dhidi ya Senegal pamoja na sare moja na Zambia.

Zambia na Tanzania zinakutana tena katika michuano hiyo, hivi sasa timu zote zikiwa na kizazi kingine cha soka. 

Michuano hiyo itafanyika kuanzia Aprili 4-25, 2020.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post