KIGWANGALLA AMUOMBA RC GAMBO AWASAMEHE WALIOSAMBAZA PICHA ZA UHARIBIFU WA BARABARA HIFADHI YA NGORONGORO


Waziri wa Maliasili na Utalii wa Tanzania, Dk Hamis Kigwangalla amewaombea msamaha waongoza utalii ambao walisambaza video kwenye mitandao ya kijamii ikionyesha uharibifu wa barabara kwenye Hifadhi ya Taifa ya Ngorongoro.


Kupitia akaunti yake ya twitter, Dk Kigwangalla ameandika kuwa amemuomba Mkuu wa mkoa wa Arusha Nchini Tanzania, Mrisho Gambo na kamati ya ulinzi kuwasamehe na kuchukulia hilo kama onyo.

Kigwangalla amesema kwa kuwa ni tukio la kwanza, amempongeza Gambo kuingilia kati suala hilo ambalo ameeleza linalinda hadhi ya nchi.

Amesema ni vema taarifa kama hizo wawe wanazifikisha mahala husika ili zipatiwe ufumbuzi na ikishindikana afikishiwe Waziri moja kwa moja.

“Ni vema taarifa za changamoto zikafikishwa kwetu kwa njia sahihi. Kama mtu hawapati watu wetu wa huko chini, mimi napatikana kila kona, sijajifungia kwenye selo na sijabadili namba zangu! Nipe taarifa zako na nakuhakikishia nitachukua hatua stahiki na kwa wakati,” ameandika Kigwangalla.

“Huwa sipuuzi taarifa wala ushauri na siangalii umetoka kwa nani. Nafanyia kazi kila kitu. Na ndiyo maana hata majangili tunawakamata kila siku. Kweli tuna uhuru wa kusema na kufanya lolote, lakini tuutumie vizuri kwa maslahi mapana ya Taifa letu. Hii ni nchi yetu sote, tuilinde, tuipende, tuijenge, tuifaidi,” ameandika.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527