MASHINDANO YA HUHESO FM VALENTINE MARATHON YAFANYIKA KAHAMA, DC MACHA ATAKA WANANCHI KUJITOKEZA KUCHANGIA DAMU KWA HIARI



Na Paschal Malulu-Kahama
Wananchi wilayani Kahama mkoani Shinyanga wameombwa kuendelea kujitolea kuchangia  damu salama katika hospitali ya halmashauri ya mji wa Kahama ili kupunguza uhaba wa damu hali ambayo imekuwa ikisababisha baadhi ya watu kufariki dunia kwa kukosa huduma ya kuongezewa damu.

Hayo yamesemwa na Mkuu wa Wilaya ya Kahama Anamringi Macha wakati akizindua mashindano ya mbio yajulikanayo “Huheso Fm Valentine Marathon” yenye lengo ya kuhamasisha uchangiaji wa damu kwa hiari yaliyoandaliwa na kituo cha Redio Huheso FM kilichopo wilayani humo.

Macha alisema kila mwananchi anao wajibu wa kujitolea kuchangia damu kwa hiari ili kusaidia kupunguza uhaba wa damu katika hospitali hiyo uliopo kwa sasa ambao umekuwa ukisababisha baadhi ya wakazi wa wilaya hiyo kufariki kwa kukosa huduma ya damu.

Alisema kila mkazi anapochangia damu anasaidia kuokoa maisha ya baadhi ya watu ambao ni nguvu kazi ya taifa huku akibainisha kuwa kwa mtu yoyote ambaye anachangia damu inaweza kusaidia hata ndugu yake wakati wowote akiugua ambapo kila aliyewahi kuchangia damu hupewa kitambulisho  kitakachomuwezesha kuongezewa damu ndugu yake au yeye mwenyewe pindi anapobainika kupungukiwa.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Huheso Fm, Juma Mwesigwa alisema lengo la mashindano hayo ni kuonesha upendo ikiwa mwezi huu wa Februari ni wa upendo hivyo wao kama redio waliamua kuandaa mashindano hayo ya mbio yakiwa na lengo la kuchangia damu katika hospitali ya Wilaya ya Kahama.

Mwesigwa alisema mashindano hayo yatakuwa endelevu kila mwaka kufanyika kwani wameona mwitikio wa wakazi wa Kahama ni mkubwa kutokana na kujitokeza kwa wingi na kuchangia damu kwa hiari kazi ambayo haikuwa rahisi.

 Aliahidi kuwa mwaka ujao wa 2021 mashindano hayo yataboreshwa zaidi ikiwa yatawekewa na zawadi kwa washindi ambapo kwa mwaka huu washindi watatu wamepatiwa medali kama nembo ya ushindi.

Mashindano hayo ya Huheso Fm Valentine Marathon yamefanyika jana Februari 15 mwaka huu katika uwanja wa taifa mjini Kahama ambapo katika zoezi la uchangia wa damu kwa hiari kwa wakazi wa Kahama jumla ya unit 40 za damu zilipatikana.

Mkuu wa Wilaya ya Kahama Anamringi Macha akizindua mashindano ya mbio yajulikanayo “Huheso Fm Valentine Marathon” yenye lengo ya kuhamasisha uchangiaji wa damu kwa hiari yaliyoandaliwa na kituo cha Redio Huheso FM kilichopo wilayani Kahama.
Mkuu wa Wilaya ya Kahama Anamringi Macha akizindua mashindano ya mbio yajulikanayo “Huheso Fm Valentine Marathon” yenye lengo ya kuhamasisha uchangiaji wa damu kwa hiari yaliyoandaliwa na kituo cha Redio Huheso FM kilichopo wilayani Kahama.




Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527