CORONA YAPEWA JINA JIPYA....WALIOFARIKI KWA VIRUSI HIVYO NI ZAIDI YA 1,100

Idadi ya watu waliofariki dunia nchini China kutokana na ugonjwa unaosababishwa na virusi vya corona imepindukia 1,113 huku maafisa wa Shirika la Afya Duniani (WHO) wakitangaza kuwa, kiwango cha maambukizi mapya bado hakijapungua.


Maafisa wa afya katika mkoa wa Hubei nchini China wametangaza leo Jumatano kuwa, katika kipindi cha masaa 24 yaliyopita watu 2,015 waliambukizwa virusi hivyo na kwamba watu 97 walipoteza maisha hapo jana.

Habari zaidi zinasema kuwa, idadi ya watu walioambukizwa virusi hivyo hatarishi kufikia sasa ni 44,653. Wakati huo huo, Shirika la Afya Duniani (WHO) limevipa virusi hivyo vya corona jina jipya la “COVID-19.”

Katika kikao na waandishi wa habari jana Jumanne mjini Geneva, Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Tedros Ghebreyesus alisema, "tumeona ni vyema tusiviite virusi hivyo jina la eneo fulani, mnyama au kundi la watu na ndiposa tukaunda neno COVID-19. 'CO' ikimaanisha corona, 'VI' ikisimamia virusi na 'D' (ugonjwa) na 19 ni mwaka wa mripuko wa virusi hivyo."

Virusi vya corona viliibuka mwishoni mwa mwezi Disemba mwaka jana 2019 katika mji wa Wuhan wa mkoa wa Hubei nchini China ambapo mbali na kuenea katika mikoa mingine 30 ya nchi hiyo, vimezikumba nchi nyingine za dunia


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527