TBS YAENDESHA MAFUNZO KWA WAFANYABIASHARA KAHAMA...DC MACHA ATAKA TBS KUSIMAMIA UBORA WA CHAKULA NA VIPODOZI


Na Adela Madyane- Malunde 1 blog Kahama
Katika kuhakikisha kuwa Watanzania wanatumia bidhaa zenye viwango vya ubora unaotakiwa kwa matumizi ya binadamu, mkuu wa Wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga, Anamringi Macha amelitaka Shirika la Viwango Tanzania kuhakikisha linasimamia ubora wa Bidhaa na si vinginevyo.

Macha alitoa agizo hilo juzi wakati akifungua Mafunzo ya siku moja kwa wafanyabiashara mbalimbali wa Wilaya ya Kahama wanaojihusisha na masuala ya ujasiliamali wa bidhaa mbalimbali yaliyoandaliwa na Shirika la Viwango Tanzania TBS yaliyofanyika mjini Kahama na kujumuisha washiriki 100 wakiwemo wauza chakula na wauzaji wa vipodozi.

Macha amesema kuwa hapa nchini Wafanyabiashara wengi wa Vipodozi wamehatarisha afya za Watanzania kwa kusambaza bidhaa ambazo hazina viwango vya Ubora unaotakiwa katika matumizi ya binadamu hali ambayo itaendelea kusababisha madhara iwapo hali hiyo haitadhibitiwa.

Macha amesema kuwa eneo hilo la vipodozi bado lina shida kubwa na kwamba linafanya ukatili wa wazi wazi kwa Watanzania kutokana na kuwauzia bidhaa ambazo hazijahakikiwa na Shirika la viwango Tanzania TBS na hivyo kusababisha madhara ya mara kwa mara kwa watumiaji.

Aidha amewataka TBS kuhakikisha kuwa wanafanya uchunguzi wa kina kwa wafanyabiashara wa vipodozi ambao bidhaa zao hazijahakikiwa na kuwa na kiwango cha ubora unaohitajika hali ambayo itaepusha madhara ya kuathhirika kwa ngozi kwa watumiaji.

Naye mfanyabiashara wa vipodozi Joseph Walioba amesema kuwa Wafanya biashara hawana elimu juu ya vipodozi licha ya hapo awali kutembelewa na maafisa kutoka TFDA na kuahidi kufanyia kazi mafunzo hayo waliyopatiwa na TBS.

“Binafsi nafanya biashara ya vipodozi vya asili na kuchakata asali na siagi vyote hivi pamoja na elimu yangu ndogo bidhaa yangu imehakikiwa na TBS kwakweli hapa nazidi kupata elimu kwakuwa nilisha anzisha biashara nyingine ya vipodozi,” amesema Ebson Muzibila.

Kwa upande wake Afisa Usalama wa Chakula mwandamizi Nuru Mwasulama amesema kwa sasa wanaendelea kutoa mafunzo katika sehemu mbalimbali ili kuwajengea uwezo wajasilamali wadogo ili wafanye biashara zisizoleta athali kwa wananchi.

Amesema kuwa lengo la mafunzo hayo ni kuwataka wajasiliamali wazalishe chakula salama ili kudumisha afya za walaji huku akizungumzia upande wa vipodozi aliwataka wafanyabiashara wa vipodozi kuzingatia kanuni za vipodozi na kuwasisitiza kuacha kuhifadhi bidhaa nje jambo ambalo linasababisha kuondoa uhalisia wake.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527