TCRA KUJA NA MSAKO KWA WALIOWASAJILIA WENZAO LAINI ZA SIMU


Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kwa kushirikiana na watoa huduma, imetangaza kufanya uhakiki wa laini zote za simu zilizosajiliwa ili kuondoa wale waliosajili kwa kutumia kitambulisho cha mtu mwingine.


Pia uhakiki huo utawahusu wale waliosajili laini zao kwa kutumia kitambulisho tofauti ambao wote watachukuliwa hatua za kisheria.

Kwa mujibu wa tangazo la mamlaka hiyo, TCRA imeamua kufikia uamuzi huo ili kujiridhisha waliosajili laini zao za simu kwa kutumia kitambulisho sahihi.

Katika tangazo hilo, TCRA ilisema kuwa kwa kushirikiana na watoa huduma itafanya uhakiki huo.

"Kusajili laini ya simu kwa kutumia kitambulisho cha mtu mwingine ni kosa sanjari na kupewa laini iliyojasiliwa na mtu mwingine.”

Tangazo hilo limesema kuwa onyo na tahadhari zitaendelea kutolewa kwa makundi yote yanayohusika na usajili wa laini hizo.

“Kwa waliositishiwa huduma za laini zao za simu kuanzia Januari 20, wanaweza kuendelea na utaratibu wa usajili kwa lengo la ama kurudisha laini hizo zilizofungwa kama zitakuwa bado zipo au kupata mpya, mchakato huu ni endelevu,” sehemu ya tangazo hilo ilisema.

Pia tangazo hilo linasema watumiaji au waombaji wapya wa laini za simu wataendelea kusajiliwa muda wowote kwa kutumia kitambulisho cha Taifa na kuhakikiwa kwa alama za vidole.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527