JESHI LA KENYA LAZIMA SHAMBULIZI LA AL-SHABAAB LAMU...WANNE WAUAWA

Jeshi la Ulinzi la Kenya (KDF) limetangaza habari ya kuwaua  wanachama wanne wa kundi la kigaidi la al-Shabaab katika kaunti ya Lamu, kusini mashariki mwa Kenya, mpakani na Somalia.


KDF imesema katika taarifa kuwa, hakuna askari au raia aliyeuawa katika shambulizi hilo lililofeli la alfajiri ya leo mwendo wa saa kumi na moja, dhidi ya kambi ya jeshi iliyoviziwa na wanamgambo wa al-Shabaab, karibu na uwanja mdogo wa ndege wa Manda, eneo la Magogoni.

Kamishna wa Kaunti ya Lamu, Irungu Macharia amethibitisha kutokea uvamizi huo ambao al-Shabaab imekiri kuhusika nao. Hata hivyo Jeshi la Ulinzi la Kenya limefanikiwa kuzima shambulizi hilo kwa kutumia ndege ya kijeshi.

Duru za habari zinaarifu kuwa, kambi hiyo ya kijeshi ina askari wa Kenya na Marekani.

Haya yanajiri siku chache baada ya wapiganaji wa kundi hilo la kigaidi kuteka nyara basi la abiria katika kaunti hiyo ya Lamu, na kuua watatu miongoni mwao.

Siku ya Ijumaa, wanamgambo wasiopungua 33 wa kundi la kigaidi la al-Shabaab waliangamizwa katika operesheni mbili tofauti za jeshi kusini magharibi mwa Somalia.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527