BINTI AUAWA KWA KIPIGO CHA SHANGAZI KISA KUCHELEWA KURUDI NYUMBANI AKITOKA KWA MPENZI WAKE


Na Amiri Kilagalila-Njombe
Jeshi la polisi mkoani Njombe linamshikilia mwanamke aliyefahamika kwa jina la Apronia Mwinuka(35) mkazi wa mtaa wa Kikula kata ya Makambako mkoani Njombe kwa tuhuma za kumpiga na kumsababishia kifo shangazi yake Elina Mwinuka (18) kwa kosa la kuchelewa kurudi nyumbani.

Kamanda wa polisi mkoa wa Njombe Hamis Issa anasema uchunguzi umebaini binti huyo amefariki kutokana na kipigo alichokipata huku ikidaiwa alichelewa kurudi nyumbani kutokana na kupitia kwa mpenzi wake.

“Alichokifanya shangazi alitoa adhabu,aliamua kutoa adhabu ya kipigo kwa huyu binti na anasema yeye alipitia kwa mtu ambaye mpenzi wake,kwa hali kama hiyo shangazi alikasirika kwanini alichelewa,na kile kipigo kilisababisha binti akafariki dunia wakati akipelekwa kupata matibabu”

Mume wa Apronia, Thadei Mhongole amesema tukio hilo limetokea wakati yeye akiwa kwenye shughuli za utafutaji na aliporudi alikuta binti huyo akiwa  amezimia baada ya kupigwa na shanganzi yake.

“Ni mtoto wa kakaangu kwa kweli kuondokewa na huyu ndugu yangu ninasikitika sana,wito wangu hasa kwa akina mama wawe na kiasi katika kuwaonya watoto”alisema Mhongole

Baadhi ya majirani wa familia hiyo wamesema kuwa mwanamke huyo amekuwa na tabia ya kuwaadhibu watoto mara kwa mara.

“Ni kawaida yake kuwaadhibu hata watoto wake mara kwa mara hata wakipoteza mkoba sasa adhabu ya juzi ikawa imezidi kipimo ikampekea mtoto kukata roho kabisa,tulipokagua kwenye nyumba yao tulikuta kuna njiti za mihanzi ambazo alikuwa anamtandikia na vipande viwili vimebanduka kabisa”alisema mmoja wa majirani

Keneth Solomon Kibiki ni mwenyekiti wa serikali ya mtaa wa Kipagamo kata ya Makambako,amekemea vitendo hivyo.

 “Tukio hili linatuhuzunisha sana viongozi na tunakemea lisijiludie kwasababu adhabu zinapitiliza mpaka tunapunguza nguvu kazi ya taifa”,alisema Keneth Solomoni.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527