MBUNGE WA MOROGORO MJINI ABDULAZIZ ABOOD AISHUKURU SERIKALI KULETA MASHINE YA X- RAY HOSPITALI YA RUFAA MKOA WA MOROGORO

Mbunge wa Jimbo la Morogoro Mjini Mhe. Abdulaziz Abood (CCM) akiangalia namna mashine ya X-ray ya kisasa inavyofanya kazi katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Morogoro.

Kufuatia kilio cha muda  mrefu cha wakazi wa  mkoa wa Morogoro juu ya kukosekana kwa mashine ya X-ray ya kisasa katika hospitali ya rufaa ya mkoa huo hali iliyokuwa ikiwalazimu kupewa rufaa kwenda hospitali ya taifa Muhimbili kwa ajili ya Matibabu hatimaye Serikali imesikia kilio chao na kupeleka mashine hiyo ya kisasa kama ilivyoahidi.

Akiendelea na ziara ya kutembelea hospitali ya Rufaa ya Morogoro na vituo vya afya katika manispaa ya Morogoro leo Alhamis Januari 16,2020, Mbunge wa Jimbo la Morogoro Mjini Mhe. Abdulaziz Abood (CCM) amejionea mashine hiyo ikifanya kazi.

Mhe. Abood ameishukuru serikali kwa kutekeleza ahadi yake hiyo na kuwajali wananchi wa mkoa wa Morogoro kwa kuleta mashine ya kisasa kwa ajili ya huduma za X-ray kwani kilikuwa ni kilio cha muda mrefu ambacho amekuwa akiiomba Serikali kuwasaidia kifaa hicho.

Mhe. Abood amesema mara kadhaa amekuwa akiomba kupatiwa mashine hiyo hata akiwa bungeni na amemshukuru Rais Magufuli kwa kusikiliza ombi hilo maalum na kuwapatia mashine hiyo ya X-ray ya kisasa.

Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Morogoro,Dkt.Ritha Lyamuya amesema mashine hiyo imekuwa msaada mkubwa kwao kutokana na kuwa na uwezo mkubwa wa kazi hali ambayo amesema imesaidia hata kupunguza malalamiko ya wagonjwa ambao walikuwa wakikosa huduma ya X-ray kutokana na mashine iliyokuwepo awali kutokuwa na uwezo wa kufanya kazi.

Dkt. Lyamuya amesema mashine hiyo ina uwezo mkubwa wa kufanya kazi na hivyo kusaidia hata kupunguza idadi ya wagonjwa ambao walikuwa wakipewa rufaa kwenda hospitali ya taifa muhimbili kwani mashine hiyo ina uwezo wa kutuma taarifa za mgonjwa kwa njia ya mtandao na kurejesha majibu ndani ya muda mfupi.
Mbunge wa Jimbo la Morogoro Mjini Mhe. Abdulaziz Abood (katikati) akipokea maelezo namna mashine ya X-ray ya kisasa inavyofanya kazi katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Morogoro.
Mbunge wa Jimbo la Morogoro Mjini Mhe. Abdulaziz Abood (katikati) akipokea maelezo namna mashine ya X-ray ya kisasa inavyofanya kazi katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Morogoro.
Mbunge wa Jimbo la Morogoro Mjini Mhe. Abdulaziz Abood (katikati) katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Morogoro.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527