WAZIRI JAFO AKUNWA NA MATUMIZI NA USIMAMIZI WA FEDHA ZA MIRADI HALMASHAURI YA MJI MBINGA


WAZIRI wa Nchi ofisi ya Rais Tamisemi Seleman Jafo,amemuagiza mkandarasi Suma Jkt anayejenga jengo la ofisi za Halmashauri ya mji Mbinga mkoani Ruvuma, awe amekamilisha kazi hiyo ifikapo tarehe 30 Desemba mwaka huu.

Halmashauri ya Mji Mbinga,imeingia mkataba na Suma JKT  kujenga jengo hilo lenye ghorofa moja kwa gharama ya shilingi bilioni 2.9 mwaka 2018 ili kurahisisha utoaji huduma na kuwaondolea adha watumishi wa Halmashauri hiyo, ambao kwa sasa wanalazimika kubanana katika jengo la idara ya ujenzi walilorithi kutoka halmashauri ya wilaya Mbinga.

Aidha Waziri Jafo, amezitaka  wa Halmashauri nyingine za mkoa wa Ruvuma,kuiga mfano wa Halmashauri ya mji Mbinga kwa kusimamia kikamilifu ujenzi wa jengo hilo sambamba na matumizi mazuri ya fedha zinazopelekwa kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo inayolenga kuchochea na kuharasisha maendeleo.

Waziri Jafo ametoka kauli hiyo mwishoni mwa wiki wakati akikagua ujenzi wa jengo  la ofisi za Halmashauri hiyo na kuwataka wakurugenzi  wengine wa mkoa wa Ruvuma kuiga utendaji, na uadilifu wa Mkurugenzi wa Mji Mbinga Grace Quintine na timu yake.

“lazima  wakurugenzi wengine waige mfano mzuri wa Mbinga Mji, ukipewa fedha basi uzitumie vizuri,Mheshimiwa Rais ametafuta  fedha za kujenga jengo hili ili watumishi mfanye kazi zenu katika mazingira bora, Mkuu wa mkoa hapa  nimeridhika na kazi iliyofanyika,kwa kweli nimefurahi sana kwani fedha zilizoletwa zimefanya kazi  nzuri nampongeza Mkurugenzi na watu wake”alisema Waziri Jafo.

Waziri Jafo alisema, baadhi ya maeneo zinapelekwa fedha lakini hakuna kazi zinazofanyika badala yake kunakuwa ubabaishaji mkubwa unaokwamisha na kuchelewesha mipango ya Serikali.

Ameitak Suma Jkt kufanya kazi usiku na mchana na kuhakikisha jengo hilo linaanza kutumika kabla ya mwisho wa mwezi Januari 2020  kwa kuwa mkataba  wake ni Mwezi Desemba 2019 na imani yake kuwa watumishi watahami  katika jengo hilo mapema.

Kwa upande wake mhandisi anayesimamia ujenzi wa jengo hilo Amos Agostine alisema, ujenzi wa jengo hilo umefikia asilimia 95 na kwamba gharama za ujenzi ni zaidi ya  Bilioni 2,983,122,246.

Amos alisema, kwa sasa wapo katika hatua za mwisho kukamilisha ujenzi huo kwa kupaka rangi,kuunganisha umeme,kujenga ngazi na shughuli nyingine ndogo ndogo.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527