BASHIRU : CCM SIO CHAMA CHA KUVUNA MAPESA


Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Dkt. Bashiru Ally, akiwa njiani kuelekea Bukoba kwa mapumziko ya siku kumi, amewaeleza wananchi kazi na misingi ya CCM ni kutoa uongozi, si kujilimbikizia pesa kama vinavyohubiri baadhi ya vyama vya siasa nchini.

Ameyaeleza hayo, aliposimamishwa na mamia ya wananchi wa kata ya Kasharunga wilayani Muleba.

"Chama chetu ni chama kikubwa, kimeanzia ngazi ya shina, unapokuwa kiongozi au mwanachama ni heshima kubwa umepewa, sisi sio wavuna mapesa kupitia kwenye uongozi, kama wanavyojinadi wengine, sisi chama chetu ni chama cha uongozi pesa inakuja kwa kuchapa kazi sio kuihubiri." Dkt. Bashiru amesisitiza.

Ameeleza pia,  umuhimu wa kuendelea kufanya kazi kwa bidii ili kutimiza malengo tuliojiwekea kuanzia ngazi ya familia na Taifa kwa ujumla.

Aidha, Dkt. Bashiru amefafanua baadhi ya malengo ya CCM katika kukuza kipato cha mwananchi mmoja mmoja ikiwa ni pamoja na  kuunganisha barabara zote kuanzia zile za mikoa, wilaya, kata hadi vijiji, upatikanaji wa mitandao ya simu, umeme, maji na huduma za afya kila kijiji.

Ambapo ameeleza kuwa, "CCM inataka maendeleo vijijini, vijiji viwe ni sehemu za uzalishaji mali na viwe ndio vitovu vya maendeleo yetu". Katibu Mkuu amesisitiza

Mapokezi hayo, yameongozwa na Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Muleba Ndg. Athumani Kahara na Mkuu wa wilaya hiyo Ndg. Richard Ruyango.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527