WAZIRI BITEKO ATOA ELIMU KWA WAFANYABIASHARA WA MADINI

Na Tito Mselem,Arusha
Waziri wa Madini Doto Biteko amewataka wafanyabiashara wa Madini ya Vito kote nchini kuhakikisha wanafanya biashara zao kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Taratibu zilizowekwa na Serikali.  


Waziri Biteko ameyasema hayo Desemba 21, 2019 wakati akizungumza na Wafanyabiashara wa Madini (Dealers na Brokers) kwenye mkutano uliofanyika katika ukumbi wa Mount Meru, jijini Arusha.

Waziri Biteko amewatahadharisha wafanyabiashara wote kwamba, wale wote wanaofanya vitendo vilivyo kinyume na taratibu zilizowekwa na serikali watachukuliwa hatua kali za kisheria.

Pamoja na mambo mengine, Waziri Biteko amesisitiza suala la Sheria na Kanuni zinazohusu masoko na uongezaji thamani wa madini ya vito pamoja na masharti ya leseni wanazomiliki.

“Nipende kueleza kwamba, wale wote wanaofanya biashara ya madini kwa kufuata Sheria na Taratibu hawatabuguziwa na mtu yoyote, hivyo niwaombe wadau wote waa madini kufuata taratibu”, Waziri Biteko alisema.

Wakati huo huo, Waziri Biteko, amevitaka vyama vyote vya madini nchini kushirikiana na kupendana katika biashara ya madini na kueleza, kwamba, kwenye biashara ya madini kuna majungu mengi ambayo hayana tija.

Aidha, Waziri Biteko amevipongeza vyombo vya ulinzi na usalama kwa kazi nzuri wanazozifanya katika kusimamia na kulinda rasilimali madini nchini.

“Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli anawapenda sana wafanyabiashara na wachimbaji wa madini lakini anachukizwa sana akisikia kwamba kuna mtu amekamatwa akitorosha madini au anakwepa kodi ya serikali,” alisema Waziri Biteko.

Awali, Waziri Biteko alitembelea soko la Madini la jijini Arusha na kuwapongeza wafanyabiashara wote wa madini kwa kufuata agizo la serikali la kuhamishia shughuli za madini katika soko hilo.                        

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu, Anthony Mavunde, amesema Nchi inawahitaji wataalamu wa madini kwa asilimia kubwa na kuanzia mwakani Wizara yake itaanza kuweka mikakati ya upatikanaji wa vibali vya ajira kwa wageni kwa haraka.

Nae, Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo, amempongeza Waziri wa Madini Doto Biteko, kwa usimamizi mzuri wa Rasilimali Madini nchini na juhudi kubwa anazo zifanya katika kutatua changamoto wanazozipitia wafanyabiashara na wachimbaji wa madini nchini.

“Nichukue fursa hii, kuwataka wadau wote wa madini nchini kumuunga mkono Waziri wa Madini kwa kufuata Sheria naTaratibu zilizowekwa na serikali na kuachana na suala la kutorosha madini,” Gambo alisema.

Pia, Mwenyekititi wa Tume ya Madini, Prof. Idris Kikula, amesema Tume ya Madini imejipanga kikamilifu kuhakikisha leseni zinatolewa kwa wakati kwa waombaji na kuimarisha usimamizi wa Masoko ya Madini nchini.

Nae, Mkurugenzi wa Huduma za Sheria wa Wizara ya Madini, Edwin Igenge ameeleza kwamba Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2017 inatoa mwongozo kwa shughuli zote za madini nchini na kuwataka wadau wote wa madini kusoma Sheria mpya ya madini ili waelewe miko na taratibu za shughuli hiyo.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527