BOEING YATANGAZA KUACHA KUZALISHA NDEGE ZA 737 MAX


Kampuni ya Boeing itasimamisha kwa muda uzalishaji wa ndege zake zilizokumbwa na matatizo za 737 Max mwezi Januari.

Utengenezaji wa ndege hizo ulikuwa ukiendelea licha ya ndege za chapa hiyo kuzuiwa kupaa kwa mezi tisa baada ya kuhusika katika ajali mbili zilizosababisha vifo vya mamia ya watu.

Zaidi ya watu 300 walipoteza maisha wakati ndege mbili za 737 Max zilipoanguka katika nchi za Indonesia na Ethiopia baada ya kuripoti matatizo katika mfumo wake mpya.

Boeing imekua ikitumaini kuwa ndege hizo zitarejea tena angani kufikia mwishoni mwa mwaka huu.

Hata hivyo wasimamizi wa safari za anga nchini Marekani wamesema wazi kuwa ndege hizo hazitapewa kibali cha kurejea angani katika siku za hivi karibuni.

Kampuni ya Boeing, yenye makao yake Seattle, Washington ni moja ya wauzaji wakubwa zaidi wa ndege duniani.

Kampuni hiyo imesema katika taarifa yake kwamba haitawafuta kazi wafanyakazi wanaofanya kazi na 737 Max, lakini kusimamishwa kwa utengenezaji zake kunaweza kuwaathiri wasambazaji na uchumi kwa ujumla.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527