WANANCHI ITUMBO WAOMBA UJENZI WA ZAHANATI UKAMILIKE KUZUIA VIFO VYA AKINA MAMA WAJAWAZITO USHETU


Naibu waziri wa Ujenzi, Elias Kwandikwa na mwenyekiti wa CCM wilaya ya Kahama Thomas Myonga wakifurahia baada ya kuona mwitikio mzuri wa uchangiaji wa maendeleo kwa wananchi wa kijiji cha Itumbo.
Naibu Waziri wa Ujenzi, Elias Kwandikwa,akiongozana na mwenyekiti wa CCM wilaya ya Kahama Thomas Myonga kukagua jengo la Zahanati ya Itumbo iliyojengwa kwa nguvu za wananchi.
Baadhi ya wananchi wakimsikiliza Naibu waziri wa Ujenzi, Elias Kwandikwa,katika hafla hiyo ya uchangiaji wa ujenzi wa Zahanati.
SALVATORY NTANDU

Wakazi wa kijiji cha Itumbo kata ya Kisuke wameiomba Halmashauri ya Ushetu mkoani Shinyanga kukamilisha ujenzi wa jengo la zahanati ya kijiji hicho ili kuzuia vifo vya akinamama wajawazito na watoto kutokana na kutembea umbali wa kilomita 12 kufuata huduma ya afya.

Hayo yamebainishwa jana Sofia Lazaro na Emiliana Mohamed katika hafla maalum ya uchangiaji wa fedha kwaajili ya ukamilishaji wa zahanati hiyo ulioongozwa na Naibu waziri wa Ujenzi, na mbunge wa jimbo la Ushetu, Elias Kwandikwa uliofanyika katika kijiji hicho.

“Akinamama wajawazito katika kijiji hicho wamekuwa wakifungulia njiani kutokana na kusafiri umbali mrefu ambapo wengine hulazimika kulipishwa shilingi elfu 6000 kwa usafiri wa pikipiki kwa mchana na kwa nyakati za usiku bei hungezeka hadi kufikia elfu 1000”,alisema Lazaro.

“Tumelazimika kuchanga fedha zao ili kusogeza huduma hiyo ambapo kwa sasa huduma za matibabu huzipata kutoka katika zahanati ya kijiji cha kisuke na wakati mwingine hulazimika kwenda katika hopitali ya Halmashauri ya mji wa Kahama ambayo ipo umbali wa kilomita 40”,alisema Mohamed.

Akijibu hoja za wakazi hao ,Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri hiyo Michael Matomora  alisema wametenga shilingi milioni 60 kwaajili ya kulikamilisha jengo la zahanati hiyo huku hospitali ya wilaya ya Ushetu ikitarajia kuanza kutoa huduma za matibabu Januari 2020.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Ujenzi Elias Kwandikwa alisema serikali ya awamu ya tano inaendelea na ujenzi mbalimbali wa majengo ya zahanati na vituo vya afya katika jimbo hilo ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma karibu.

“Ilani ya uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) imeainisha kuwa kila kijiji ni lazima kiwe na zahanati na Kata lazima iwe na kituo cha afya, sisi kama wasimamizi wa ilani hii tutahakikisha utekelezaji wake unafanyika kwa haraka”Alisema Kwandikwa

Ujenzi wa zahanati hiyo ulianza mwaka 2010 na katika harambee hiyo Benki ya NMB walitoa ahadi ya bati 170 huku zaidi ya mifuko 80 saruji mifuko 80 ikichangwa na wadau mbalilmbali wamaendeleo na fedha zaidi ya shilingi milioni 10 zilipatika katika harambee hiyo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527