CHAUMMA NAO WATANGAZA KUTOSHIRIKI UCHAGUZI ...HASHIM RUNGWE ASEMA ' UCHAGUZI UMETAYARISHWA KWA HILA'



CHAMA cha Ukombozi wa Umma (CHAUMMA), kimetangaza kutoshiriki Uchaguzi wa Serikali za Mitaa. 

Uamuzi huo umetangazwa leo tarehe 9 Novemba 2019 na Hashim Rungwe, Mwenyekiti wa CHAUMMA Taifa, wakati akizungumza na wanahabari jijini Dar es Salaam. 

Rungwe ameeleza kuwa, wamejitoa katika uchaguzi huo kwa kuwa mchakato wake ulikuwa na hila, kwa wagombea wa vyama vya upinzani.

“Tunashindwa, tunaona kwamba huu uchaguzi umetayarishwa kwa hila, kwamba wananchi wasishiriki. Tunaona kwamba uchaguzi huu umefanywa hila. Na sisi pia tunaamua hatutashiriki uchaguzi huu. Tunaomba wagombea wetu popote walipo wasishiriki,” ametangaza Rungwe.

Rungwe amesema wamefikia hatua hiyo, baada ya kuona jitihada zao za kutafuta suluhu kuhusu hujuma hizo, kugonga mwamba.

“Wanachama wote wafahamu huu uchaguzi una hila, tumekata rufaa lakini haijasaidia chochote. Kama wao ndio wanataka hivi, kwamba wale wana nguvu, wana dola, sisi hatuko tayari kupigana,” amesema Rungwe na kuongeza;

“Watanzania hatuko tayari kupigana. Hatuna tabia hiyo. Unatuzuia hatufanyi siasa. Sasa uchaguzi halali umeutangaza tumekuja kuchukua fomu, matatizo tunasumbuliwa, tumezirudisha zimekataliwa, tufanye nini.”

Rungwe amesema wananchi ambao ndio wapiga kura, wataamua la kufanya kuhusu uchaguzi.

Rungwe amesema CHAUMMA kilisimamisha wagombea zaidi ya 250, ambapo jiji la Dar es Salaam kilisimamisha wagombea 5, Morogoro (38), Iringa (30), Njombe (20) Tabora (38), Kigoma (10), Mwanza (25), Mara (40), Mtwara (7), Tanga 10 na Shinyanga (6).

CHAUMMA kinakuwa chama cha tatu kuususia uchaguzi huo, baada ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na ACT- Wazalendo, kutangaza kujiondoa.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527