RAIS MAGUFULI AWAPA POLISI OFISI YA MAKAO MAKUU DODOMA YENYE GHOROFA NNE


Rais Dk. John Magufuli, amewapa ofisi jeshi la polisi jijini Dodoma ikiwa ni sehemu ya jeshi hilo na serikali kuhamia jijini humo.

Akizungumza katika uzinduzi wa ujenzi wa nyumba za polisi eneo la Nzuguni jijini Dodoma leo Ijumaa Novemba 22, amesema anawakabidhi jengo la ghorofa nne lililokuwa linatumiwa na Uwasa ambapo yatakuwa makao makuu ya jeshi hilo.

“IGP nimefurahi umesema umehamia hapa Dodoma, ningeshangaa kuona mimi nimehamia hapa wewe bado hujahamia, ningeteua IGP wangu wa hapa Dodoma.

“Lakini kwa sababu umewahi umehamia hapa nakushukuru na kwa sababu umehamia kufanya hivyo kwa sababu askari hasubiri nyumba nimeamua kuwapa zawadi, siyo hela mimi sitoagi hela nimeamua kwa vile mmeshatekeleza wito wa kuhamia hapa na sitaki kujua mmehamia wapi inawezekana  mnakaa kwenye miembe kwenye nini, lakini jukumu lenu mmelifanya la kuhamia hapa nimewamua kuwapa jengo moja kubwa lenye ghorofa nne lilikouwa linatumiwa na Uwasa.

“Sasa ndiyo yatakuwa Makao Makuu ya Polisi na ninakupa picha zenyewe ni matumaini yangu leo nitaona makao makuu ya polisi kwenye jengo hilo,” amesema Rais Magufuli.

Pamoja na mambo mengine, Rais Magufuli amesema serikali imeshahamia Dodoma hakuna lugha nyingine kwamba watahamia, hapa ndiyo makao makuu hakuna jingine na watabanana hapa hapa kwa wagogo hakuna namna.

“Dodoma inapendeza, Dodoma inavutia. Na katika miaka michache ijayo jiji hili litaipita hata jiji la Dar es Salaam na majiji mengine,”- amesema.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527