MWENYEKITI WA CHADEMA FREEMAN MBOWE NI MGONJWA....KALAZWA AGA KHAN

Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) nchini Tanzania, Freeman Mbowe anaumwa na amelazwa katika Hospitali ya Aga Khan, jijini Dar es Salaam tangu Novemba 17, 2019.

Mbowe ni miongoni mwa viongozi tisa wa Chadema wanaokabiliwa na kesi ya uchochezi namba 112/ 2018 inayoendelea leo Jumanne Novemba 19, 2019 kwa hatua ya utetezi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Alitakiwa kuendelea kujitetea leo lakini mdhamini wake, Greyson Selestine ameieleza mahakama hiyo kuwa mbunge huyo wa Hai anaumwa na amelazwa katika hospitali hiyo.

“Mbowe amelazwa tangu Novemba 17 katika hospitali ya Aga Khan,” amesema Selestine bila kueleza mwenyekiti huyo wa Chadema anaumwa nini.

Kinachoendelea katika kesi hiyo ni washtakiwa wanne, mbunge wa Tarime Vijijini, John Heche; Ester Bulaya (Bunda), Mchungaji Peter Msigwa (Iringa Mjini) na Halima Mdee (Kawe) kujitetea kwanini wasifutiwe dhamana.

Ijumaa iliyopita Novemba 15, 2019, mahakama hiyo ilitoa amri ya kukamatwa kwa washtakiwa hao kutokana na kukiuka masharti ya dhamana baada ya kutofika mahakama kusikiliza kesi hiyo.

Via Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527