MBOWE AMJIBU NDUGAI UTORO BUNGENI ......'KWANI NIMEKUWA MCHAWI NIWEPO MAHAKAMANI NA BUNGENI NIWEPO?'

Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe amemjibu Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai aliyedai kuwa mbunge huyo wa Hai ni mtoro bungeni.

Akizungumza na Mwananchi leo Ijumaa Novemba 15, 2019 Mbowe amesema yeye pamoja na wabunge wengine sita wa chama hicho hawapo bungeni kwa kuwa wanahudhuria kesi inayowakabili katika mahakama ya hakimu mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam.

Jana Alhamisi Novemba 14, 2019 bungeni mjini Dodoma, Ndugai alisema kambi hiyo inakosa nafasi za mara kwa mara kuuliza maswali kwa Waziri Mkuu kwa sababu ya utoro wa Mbowe.

Amesema katika kipindi hicho swali la kwanza huulizwa na kiongozi wa kambi hiyo.

“Bunge linaendelea na vikao bungeni na huku mahakama inaendelea kusikiliza kesi inayotukabili sasa anategemea ni mbunge gani atakuwepo kila mahali kwani mimi nimekuwa mchawi huku niwepo na kule niwepo,” amesema Mbowe.

Mbowe na viongozi wengine wanane wa Chadema kwa pamoja wanakabiliwa na mashtaka 13, ikiwemo kula njama, kufanya mkusanyiko wenye ghasia na kuhamasisha hisia za chuki.


Via Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527