LUGOLA ATOA ONYO KWA WATAKAOFANYA VURUGU UCHAGUZI SERIKALI ZA MITAA


Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola amewataka Makamanda wa Polisi nchini kusimamia kampeni zilizoanza za Uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwa kuwalinda wagombea wa vyama vya siasa ambavyo vilitangaza kujitoa, pamoja na kuwashughulikiwa bila huruma watu waliopanga kufanya vurugu. 

Waziri Lugola amesema ana taarifa za kutosha kuhusu baadhi ya watu waliopanga kufanya vurugu wakati wa kampeni kwa lengo la kuvuruga uchaguzi huo, aliwataka Makamanda hao kuwasaka kila kona, kuwakamata watu hao ambao wana nia mbaya ya kuvuruga uchaguzi huo.

“Nawataka mtende haki katika usimamizi wa uchaguzi huu, lakini wapo baadhi ya watu ambao wamepanga kufanya vurugu, watu hao msicheke nao, watu hao washughulikieni bila huruma, na badala ya kuwamwagia maji ya kuwasha, sasa watumbukizeni ndani ya tenki la maji hayo ili waweze kuwashwa zaidi, hatutaki vurugu, tunataka amani na utulivu ndani ya nchi yetu,” Lugola.

Kwa upande wa Vyama vya Siasa vilivyojitoa kushiriki uchaguzi huo, Lugola alisema wagombea wapo ambao wamekataa agizo hilo la vyama vyao, hivyo wameamua kushiriki uchaguzi huo wakigombea nafasi walizoziomba, hivyo wanapaswa kulindwa kwa nguvu zote kwani ni haki yao kugombea.

“Wameweka mpira kwapuni, lakini wachezaji wapo uwanjani bado wanataka kucheza,bado wanaenda uwanjani kuwapiga wachezaji hao wasiweze kucheza, bado wanataka kuwapiga waamuzi wasiweze kutoa pointi tatu muhimu kwa timu ambayo imeendelea kucheza,  hao muwashughulikie kiisawasawa,” Lugola.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527