DARAJA LA KUTISHA LAFUNGWA...LIMEJENGWA KWA VIOO

Mkoa mmoja nchini China umefunga maeneo 32 ya kuvutia watalii yaliyojengwa kwa kioo - ikiwa ni pamoja na madaraja, njia za kutembea kwa miguu na maeneo ya kujionea kwa umbali mandhari ya kupendeza  ili kutoa nafasi ya uchunguzi wa usalama wa maeneo hayo.

Maeneo 24 yaliyojengwa kwa kutumia kioo katika mkoa wa Hebei, yamefungwa tangu mwezi Machi mwaka 2018, kwa mujibu wa kituo cha televisheni cha kitaifa CCTV.

Hatua hiyo iliwahi kuripotiwa siku zilizopita.

China imeshuhudia ongezeko la ujenzi wa kutumia kioo katika maeneo ya kuvutia watalii kote nchini- lakini ajali zimeripotiwa katika maeneo hayo huku watu wawili wakipoteza maisha.

Inakadiriwa kuwa madaraja 2,300 ya vioo yamejengwa China. kwa mujibu wa chombo cha habari cha kitaifa ECNS.

Ujenzi wa kutumia kioo katika maeneo ya kuwavutia watalii ni juhudi ya nchi hiyo kuvutia watalii wa ndani ili kuimarisha sekta hiyo ambayo imekuwa ikikua kwa kasi.

Daraja la Zhangjiajie katika mkoa wa Hunan- ambalo lilikuwa daraja ndefu zaidi la kioo duniani lilifunguliwa mwaka 2016 - inasemekana ndio liliibua mshawasha wa kuendelea na mtindo huo wa ujenzi.Daraja la Hongyagu katika mkoa wa Hebei

Lakini mapema mwaka huu, mtalii mmoja alifariki na wengine sita kujeruhiwa baada ya kuteleza kutoka kioo na kuanguka katika mkoa wa Guangxi.

Mvua ilichangia njia hiyo iliyojengwa kwa kutumia glasi kuwa telezi kupita kiasi, hali iliyomfanya mwanamume mmoja kuteleza kuuanguka kupitia eneo la kujishikilia.

Alifariki kutokana na majeraha mabaya ya kichwa.

Daraja la kioo la Hongyagu- ambalo hadi mwezi Mei mwaka huu lilikuwa daraja refu zaidi la kioo duniani - ni miongoni mwa yale yaliyofungwa katika mkoa wa Hebei.

Hatua hiyo imeathiri mkoa wa Hebei pekee.

Mapema mwaka huu, serikali iliagiza mamlaka katika mkoa huo kufanya "uchunguzi wa kiusalama" kuhusu mradi wa ujenzi wa kutumia vioo.

Katika mtandao wa kijamii wa Weibo, watu wengi wamepongeza hatua ya kufungwa kwa maeneo hayo, huku mmoja akisema "wakati umewadia kuangazia suala la usalama wa maeneo hayo".

Wengine walikosoa ujenzi wa daraja kwa kutumia glasi ambao umetia fora katika miaka ya hivi karibuni.
Maelfu ya watu wakitembea juu ya daraja ndefu zaidi duniani la kioo katika mkoa wa Hebei, China

"Sielewi kwanini kuna madaraja mengi ya vioo siku hizi. Huu ni uharibifu wa fedha," alisema mtu mmoja.

Kifo kilichokea katika mkoa wa Guangxi ndicho cha pekee kuwahi kuripotiwa katika maeneo ya kuwavutia watalii yaliyojengwa kwa vioo.

Mwaka 2017, mtalii moja alifariki baada ya kuhusika katika ajali akitembea juu ya daraja la kioo mjini Hubei.

Na mwaka 2016, mtu mmoja alijeruhiwa baada ya kugongwa na mawe akitembea kwenye njia iliyojengwa kwa kioo katika mji wa Zhangjiajie.

Mwaka 2015, njia ya kioo katika mkoa wa Henan ilipasuka licha ya kufunguliwa kwa Umma mara mbili kwa wiki, hali iliyowafanya watalii kukimbia kwa hofu.
Chanzo - BBC

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527